MKURUGENZI Mtendaji wa kituo cha msaada wa kisheria cha Parallegal, Morogoro, Frola Masoi ameitaka jamii kuzingatia na kuzifuata sheria zilizopo kwenye katiba ya Tanzania zinazoitaka kuacha matendo ya ukatili wa kijinsia ili kukomesha vitendo hivyo, anaandika Christina Haule.
Masoi amesema, zipo sheria kwenye katiba ya Tanzania zinazosema binadamu wote ni sawa, kila mtu ana haki, sambamba na matamko na mikataba mbalimbali ikiwemo ya kimataifa ambayo imeridhiwa inayopinga masuala ya ukatili wa kijinsia ukiwemo mkataba wa kimataifa wa CEDAU, hivyo jamii haina budi kuzingatia.
“Licha ya Serikali ya Tanzania kutokuwa na sheria mahususi ya kupambana na ukatili wa kijinsia kwa ujumla ambayo hadi sasa watetezi wa masuala ya kijinsia wanaendelea kuipigania iwepo lakini zipo sheria hizo zinzopambana na masuala ya makosa ya kujamiiana ambazo pia kisheria zinasimama kutetea masuala ya ukatili wa kijinsia (GBV) kwa ujumla,” amesema.
Naye Ofisa Ufuatiliaji wa kituo hicho, Augustino Ernest amesema mwaka 2016 walipokea kesi 246 kutoka kwa wakazi wa manispaa pekee huku tayari wameshapokea kesi 229 katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Mei mwaka huu 2017.
Amesema, ongezeko hilo limetokana na wasaidizi wa kisheria kutembea wilaya mbalimbali za mkoa wa Morogoro kuhamasisha jamii kupinga ukatili huo ikiwemo wilayani Kilosa kwa kutoa elimu na kufanya matukio hayo kuonekana kuongezeka.
Leave a comment