Friday , 29 March 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Ujumbe wa ACT-Wazalendo kwa taifa kuhusu uchumi & corona
Habari za Siasa

Ujumbe wa ACT-Wazalendo kwa taifa kuhusu uchumi & corona

Spread the love

Ujumbe wa ACT-Wazalendo kwa taifa kuhusu uchumi & corona

Ndugu Wananchi,

Itakumbukwa kuwa Kiongozi wa Chama Chetu alimwandikia barua Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mnamo tarehe 27 Machi 20120 kumshauri hatua mbalimbali za kuchukua ili kukabiliana na mlipuko wa virusi vya Korona.

Katika barua hiyo Chama chetu kilishauri kuwa Rais aunde Timu ya Wachumi waliobobea waliopo Serikalini na walio nje ya Serikali kufanya uchambuzi wa kina wa hali yetu na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukua.

Chama chetu hakikuishia kwenye mapendekezo tu bali pia kilichukua hatua mbalimbali za kuelimisha umma kujikinga na maambukizi ya COVID 19 kwa kuzungumza na wananchi moja kwa moja kupitia Hotuba kwa Taifa aliyoitoa Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Maalim Seif Sharif Hamad, kuundwa kwa Timu ya Chama ya kukabiliana na Korona na kutumia mitandao ya kijamii, televisheni na redio kuelemisha wananchi njia za kujikinga kwa mujibu wa maelekezo ya Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) na Wizara za Afya Tanzania Bara na Zanzibar.

Leo tutazungumza nanyi kuhusu hatua zinazopaswa kuchukuliwa na Serikali zote mbili ili kudhibiti maambukizi ya COVID 19 na kuhami Uchumi wa Taifa – Tanznaia Bara na Zanzibar.

Hali halisi kwa ufupi

Zanzibar

30% ya Pato la Taifa la Zanzibar ( GDP ) inategemea Utalii na 80% ya Mapato ya Fedha za kigeni Zanzibar yanatoka kwenye Utalii. Mwenendo wa mauzo ghafi ya wafanyabiashara ya Utalii unaonyesha kuwa makampuni mengi ya Utalii yatapoteza mpaka 85% ya mapato yao katika msimu unaokuja wa Utalii 2020/21 kulinganisha na msimu ambao umemalizika wa 2019/20. Hali hii itapelekea Biashara nyingi kufilisika na watu wengi sana kupoteza ajira zao.

Fungamanisho na Sekta ya Utalii na Sekta nyingine za uchumi kwa Zanzibar ni kubwa. Hata Wakulima na Wavuvi wataathirika na kudorora kwa Utalii kwani hawatakuwa na mahala pa kuuza mazao yao – mahoteli na migahawa imefungwa. Uchambuzi wetu unaotokana na takwimu za Benki Kuu ya Tanzania unaonyesha kuwa 63% ya Uchumi wa Zanzibar umeunganishwa moja kwa moja sekta ya Utalii hivyo kuanguka kwa Utalii ni sawa na kuanguka kwa theluthi mbili ya Uchumi wa Zanzibar.

Tunatarajia kuwa kasi ya ukuaji wa uchumi Zanzibar itakuwa hasi na hivyo Uchumi kuingia kwenye mdororo (recession) kubwa zaidi kuliko wakati wowote. Wananchi na Makampuni yatahitaji msaada wa Serikali kuliko wakati wowote. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haijachukua hatua yeyote ile ya kuhami Uchumi kutokana na janga hili la Korona. ACT Wazaelendo tutapendekeza hatua za kuchukua leo.

Tanzania Bara

Jana Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limetoa uchambuzi wake wa hali ya uchumi ya Mataifa mbalimbali ya Afrika kulingana na janga la COVID 19. IMF wanakadiria kuwa kasi ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania itashuka kutoka 6.3% mpaka 2% mwaka 2020. Hii ni kasi kubwa ya kuporomoka kwa ukuaji wa uchumi. Uchumi wa Tanzania Bara unategemea Zaidi huduma ikiwemo utalii kwa 44% ikifuatiwa na viwanda na Kilimo ambacho mchango wake kwenye GDP ni 32%.

Hata hivyo Sekta ya Utalii peke yake inachangia 26% ya Mapato yote ya Fedha za Kigeni zinazoingia nchini ambapo mwezi unaoishia Machi 2020 jumla ya Dola za Marekani 2.6 bilioni ziliingia nchini kutokana na Utalii kati ya Jumla ya Dola za Marekani 10 bilioni zilioingia nchini. Ni Dhahiri kuwa sekta ya Utalii ndio imevurugwa Zaidi na COVID 19. Hata hivyo sekta nyengine pia zitadidimia.

Tayari tumeona kuwa Usafiri wa anga umesimama haswa kwa safari za kutoka nje na hivyo kuathiri mnyororo mzima wa thamani unaofungaminishwa na usafiri wa anga. Uzalishaji viwandani pia utaathiriwa kutokana na kuanguka kwa soko la walaji nchini. Serikali ya Tanzania pia haijachukua hatua zozote iwe za kikodi, kifedha au sera za fedha za nje. Leo ACT Wazalendo tutapendekeza hatua za kuchukua ili kuhami maisha ya wananchi na kuuhami uchumi wa Taifa usianguke.

Maambukizi ya COVID 19 yameongezeka kwa kasi 

Tanzania Bara

Katika Barua ya Chama chetu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tulishauri kuwa hatuwezi kuendelea na ‘business as usual’ na hivyo lazima hatua zichukuliwe zitakazoathiri kwa kiasi Fulani shughuli za kila siku za Watanzania. Kwa mfano miji ya Mwanza, Dodoma, Arusha na Dar es Salaam tunapendekezwa ifungwe watu wasiingie wala kutoka kwa muda wa siku 30. Hata hivyo, tuwe na  ‘lockdown’ inayowiana na mazingira yetu ya Tanzania yaani yaweza kuwa partial na ikahusisha baadhi ya yafuatayo:

Watumishi wa umma katika Mikoa husika wafanyie kazi majumbani mwao: kwa kuwa watumishi wa umma wana vipato vya uhakika hili halitaathiri maisha yao. Tunapendekeza kuwa Ofisi za Umma zibakize mtu mmoja kwa Idara na kwa zile kazi ambazo hazihusishi kukutana na watu na iwe kwa zamu. Pendekezo hili pia lihusishe Mashirika yote ya Umma kwenye Mikoa tajwa.

Ofisi za Umma za kutoa huduma kwa Wananchi kama Vituo vya Huduma za Afya (hospitali) na  polisi waendelee na kazi kwa kupewa vifaa maalumu vya kuzuia maambukizi ya virusi vya COVID 19.

Kumbi za starehe, shughuli za michezo na maeneo ya vinywaji kama vile na vilabu vya Pombe visimame.

Watoa huduma za vyakula kama vile Mama Lishe waendele na shughuli zao kwa uangalifu mkubwa na inapobidi watumike kusambaza vyakula majumbani kwa watu watakaohitaji msaada.

Masoko ya mazao yawe wazi kwa usimamizi maalum wa uongozi wa soko na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuweka utaratibu maalumu wa wananchi kuhemea. Masoko ambayo hayatafuata maagizo yafungwe bila kuchelewa.

Vyombo vya Usafiri viendelee kwa maelekezo maalumu ya kuhakikisha kuwa hakuna msongamano kwenye viti. Tunapendekeza kuwa magari ya jeshi yatumike kupakia abiria kuondoa msongamano

Tunarudia pendekezo letu la kupunguza msongamano magerezani kwa kuwapa dhamana watu wote wenye makosa yenye dhamana, kuwapa dhamana watu wote ambão kesi zao upelelezi bado unaendelea, kuwaachia huru watu wote wenye umri unaozidi miaka 65, Wanawake wenye Watoto na Wanawake wenye Watoto wadogo magerezani.

Tunapendekeza kuwa hospitali binafsi zenye uwezo kuwa sehemu ya karantini na isolation kuepusha kuelemewa kwa vituo vya umma vilivyopo sasa. Wako watu wenye uwezo wako tayari kulipia kukaa hospitali wanazozipenda wao wakiugua Corona. Muhimu tuhakikishe hizo hosp zinakidhi vigezo na masharti.

Msaada kwa Wananchi

Kwa kuwa hatua tulizopendekeza zitaathiri watu wasio na ajira rasmi ambao ndio wengi hapa Tanzania tunapendekeza kuwa Serikali ichukue hatua ya kuwalipa watu wote ambao hawamo kwenye ajira Rasmi ili waweze kuendelea na maisha kwa muda huo wa kuwafungia ndani (lockdown).

Fedha kutoka Akiba ya Fedha za kigeni (Gross Official Reserve) – Kwa mujibu wa Taarifa ya Benki Kuu ya Mwezi Machi, 2020 Tanzania ina akiba ya Jumla ya Dola za Marekani 5.5 Bilioni. Tunapendekeza kuwa nusu ya akiba hii itumike kuwalipa wananchi ili waweze kujikimu wakati nchi imefungwa.

Hesabu zetu zinaonyesha kuwa iwapo Tanzania Bara nzima itakuwa kwenye Lockdown, Kila Kaya ya Tanzania inaweza kulipwa Shs 300,000 kila Mwezi kwa miezi miwili na tutatumia Dola za Marekani 2.3 Bilioni tu, chini ya nusu ya Akiba yote. Kama nchi tunaweza kumudu gharama za miji inayopendekezwa. Tunapendekeza kuwa Wakazi wa Mwanza, Dar es Salaam, Arusha na Dodoma walipwe Shs 300,000 kwa Mwezi ambao Miji yao itakuwa kwenye lockdown. Malipo haya hayatawahusu watu waliopo kwenye ajira rasmi.

Sekta Binafsi ya Tanzania imeumizwa sana na mlipuko wa Korona na hivyo haitakuwa na uwezo wa kulipa Wafanyakazi wake. Tunapendekeza kuwa katika kipindi cha miezi 3 kuanzia Mei mpaka Agosti, Wafanyakazi wote kwenye sekta Rasmi walipwe Mishahara yao kutoka Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama Fao la Kukosa Ajira. Hii itawezesha Makampuni kuondokewa na gharama kubwa za uendeshaji na hivyo kuweza kuwekeza afya na kuinuka baada ya Korona kuondoka nchini. Pia hii itawezesha Wafanyakazi kutofukuzwa kazi.

Benki Kuu ya Tanzania ielekeze Mabenki yote nchini ambayo yamekopesha Watu mikopo binafsi (personal loans) yaache kukusanya marejesho ya mikopo ya watu binafsi kwa muda wa miezi 3 kuanzia Aprili, 2020.

Mamlaka ya Mapato Tanzania isikusanye kodi ya makampuni kwa makampuni ya Utalii mpaka Oktoba 2020.

Zanzibar

Kutokana na hali ya Visiwa ya Zanzibar tunapendekeza kuwa Zanzibar yote iwe kwenye lockdown kwa muda wa Mwezi mzima. Shughuli muhimu tu kama za Hospitali, Ulinzi na Usalama na shughuli za kiserikali zisizoepukika ndio ziendelee. Shuhguli za Masoko ya bidhaa za wananchi kutumia ziwekewe ratiba maalumu chini ya Usimamizi wa Serikali kuruhusu wananchi kununua chakula.

Tunapendekeza kuwa Serikali itoe msaada kwa Wananchi wakati wa lockdown ya Zanzibar; Kila Kaya Zanzibar ilipwe shilingi 300,000 kutoka mgawo wa Zanzibar katika Akiba ya Fedha za kigeni za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kutokana na idadi ya Watu Zanzibar na Wastani wa idadi ya Kaya Serikali itatumia Shilingi 128 bilioni tu, ambazo ni kiwango kidogo kulinganisha na akiba iliyopo ya Dola za Marekani Milioni 550.

Wafanyakazi wote wanaochangia kwenye Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) walipwe mshahara wao wa miezi mitatu kutoka mfuko huo. Hii itasaidia Kampuni kuepuka gharama kubwa za uendeshaji na hivyo kutopunguza Wafanyakazi. Kwa hatua hii pia Makampuni hayatalipa michango ya Hifadhi ya Jamii, SDL n.k.

Marejesho ya Mikopo ya watu binafsi kwenye mabenki yasimame kwa muda wa miezi 3. Mamlaka ya Mapato na Bodi ya Mapato Zanzibar isikusanye Kodi ya Mapato (corporation tax) mpaka kuanzia tarehe 1 Oktoba, 2020.

Hitimisho

Tunatambua kuwa Hatua hizi zinahitaji Fedha. Tumeonyesha wapi pa kupata fedha za kuwasaidia wananchi kipato kipindi cha lockdown. Tanzania inaweza kutumia mpaka shilingi trilioni 5 bila kuathiri kiwango kinachotakiwa cha akiba za Fedha za kigeni. Vile vile Mifuko ya Hifadhiya Jamii inazo fedha za kutosha kurejesha Fedha kwa Wafanyakazi kwa miezi 3 tu ya wakati huu mgumu.

Tunatambua kuwa madhara ya Korona ni pamoja na Serikali kukosa mapato kutokana na ukweli kuwa shughuli za uchumi zitaanguka. Mwenyekiti wetu wa Chama, katika hotuba yake kwa Taifa alipendekeza kuwa Serikali ya Tanzania iombe walioikopesha kusitisha kuhudumia Deni lao kwa muda wa mwaka Mmoja.

Hatua hii itaifanya Serikali kubakia na Zaidi ya Shilingi Trilioni 4 ambazo inazalipa nje kila mwaka kuhudumia Dni la Nje. Tunaisihi Serikali ya Tanzania kushirikiana na Nchi nyengine ili kupata ahueni hii ya Madeni ambayo itaweza kutumika kuhami uchumi na kujenga upya sekta ya Afya.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Chadema yamtaka Rais Samia aunde tume kuchunguza mauaji mgodi wa Barick

Spread the loveRAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, ameombwa aunde tume huru kwa...

Habari za SiasaMakala & Uchambuzi

Nani anasema kuna hasara ATCL?

Spread the loveRIPOTI za makusanyo na matumizi ya fedha katika Kampuni ya...

Habari za SiasaTangulizi

CAG: Wastaafu, wenza wao chanzo NHIF kufilisika

Spread the loveRIPOTI ya ukaguzi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu...

Habari za SiasaTangulizi

Vikundi hewa 851 vyalamba bilioni 2.6 mikopo ya halmashauri

Spread the loveVIKUNDI hewa vya wajasirimali wadogo 851 kutoka katika halmashauri 19...

error: Content is protected !!