MKURUGENZI Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa, amesema mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) kipande cha Makutupora- Tabora kitagharimu Sh 4.6 trilioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Tabora … (endelea).
Kipande hicho chenye urefu wa kilomita 368 kitajengwa na Mkandarasi Yarp Markezi kutoka nchini Uturuki ambaye ndiye anayejenga vipande viwili vya Dar es Salaam-Morogoro na Morogoro- Makutupora.
Akitoa taarifa ya mradi huo leo Jumanne tarehe 12 Aprili 2022 kwenye hafla ya uwekeaji jiwe la msingi wa kipande hicho, Kadogosa amesema ujenzi wake utakuwa wa miezi 42 na wiki nne za majaribio na unatarajiw kukamilika Oktoba 2025.
Amesema mradi utakuwa na Madaraja makubwa 32 vivuko vya juu 12 na vya chini 15 , vivuko vya mifugo, wanyama na binadamu 49 na vituo vinane vya Manyoni Itigi, Kazikazi, Tula, Malongwe, Gowekwe, Igalula na Tabora.
Amesema ujenzi utafanywa kwa mfumo wa usanifu na ujenzi na kuwatoa hofu wananchi wote watakaopitiwa na mradi huo kuwa watalipwa fidia zao.
Amesema ujenzi utafuata viwango vya kimataifa kama vipande vingine ikiwemo mwendo kasi wa 160 kilomita kwa saa kwa treni ya abiria na kilomita 120 kwa saa upande wa mizigo.
Kadogosa amesema hadi sasa serikali imeshasaini mikataba ya Sh 14.72 trilioni katika vipande vinne na tayari Sh 6.13 trilioni imeshalipa kwa mkandarasi na hadai pesa yeyote.
Ameongeza kuwa katika fedha zilizolipwa kwa mkandarasi, Serikali imeshapata kodi ya Sh 441 Bilioni kutokana na utekelezaji wa maradi.
“Tutahakikisha unatekelezwa kwa viwango na thamani ya fedha,” amesema Kadogosa.
Amesema mkataba huo ni mzuri kwani hauruhusu mkandarasi kuongeza gharama za mradi endapo kutatokea mabadiliko ya bei za vifaa, “makataba hauruhusu Mkandarasi kutuambia bei za mafuta au chuma zimepanda hivyo anaongeza gharama za mradi.”
Ameeleza kuwa endapo mikataba hiyo ingerehusu hilo hadi sasa mradi wa reli hiyo ungeshaongezeka kwa kiasi cha Sh 1.4 trilioni.
Leave a comment