WAZIRI Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameutaka uongozi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), kuhakikisha wanakamilisha kazi iliyosalia ya ujenzi wa nyumba za makazi eneo la Magomeni Kota, Dar es Salaam. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Majaliwa ametoa kauli hiyo leo Jumatatu tarehe 20 Aprili 2021, mara baada ya kutembelea mradi huo.
Amesema amefurahi kukuta majengo yamekamilika na kwamba ameridhika na maendeleo ya ujenzi wake.
Majaliwa amesema, Serikali ipo imara na miradi yote ya kimkakati inaendelea kujengwa, hivyo Watanzania waendelee kuwa na imani nayo.
Amesema, Serikali inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ipo makini na inaendelea kuwatumikia Watanzania, “tuendelee kuchapa kazi.”
“Siri ya kuwepo mafanikio na maendeleo nchini ni utulivu na amani. Tulianza vizuri tangu Serikali ya Awamu ya kwanza, tutaendelea kuimarisha amani na utulivu,” amesema.
Majaliwa ametumia fursa hiyo, kuwaasa Watanzania watumie muda mwingi kufanya shughuli za maendeleo kuliko mambo mengine yasiyo na tija.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa TBA, Daud Kondoro amesema, mradi huo una jumla ya block tano na ambazo zinauwezo wa kuchukua familia 656.
Amesema mbali na ujenzi wa nyumba hizo za makazi, pia katika eneo hilo wanajenga maduka makubwa pamoja na vizimba kwa ajili ya wajasiriamali kufanya biashara.
Mradi ulianza kutekelezwa mwaka 2016 na unatarajiwa kukamilika Mei 2021. Hadi sasa umefikia asilimia 94 ya utekelezaji wake na gharama yake ni Sh.50 bilioni.
Baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba za makazi za Magomeni Kota, Waziri Mkuu alikagua kituo cha Reli ya Kisasa cha Tanzanite jijini Dar es Salaam.
Leave a comment