WIZARA ya Ujenzi na Uchukuzi, imeeleza kwamba itakaa meza moja na Wizara ya Madini pia Kampuni ya Barrick ili kujadili ujenzi wa Barabara ya Geita – Bukoli hadi Kahama. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
“Kwa sasa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Wizara ya Madini zinaendelea na mazungumzo na Kampuni ya Barrick kuhusu utaratibu wa ujenzi wa barabara hii,” amesema Dk. Leonard Chamuriho, Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi.
Dk. Chamuriho ametoa kauli hiyo leo tarehe 16 Aprili 2021, bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Kasimu Iddi Iddi, Mbunge wa Msalala, aliyetaka kujua ni lini serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Geita – Bukoli hadi Kahama kwa kiwango cha lami?
Amesema, wizara hiyo kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), imekamilisha kazi ya upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na maandalizi ya makabrasha ya zabuni kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 139 inayounganisha mikoa ya Geita na Shinyanga.
“Kazi hii ilifanywa na Mhandisi Mshauri M/s ENV Consult (T) Ltd kwa gharama ya Sh. 440 milioni. Kwa sasa serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
“Aidha, kampuni ya uchimbaji madini BARRICK imeonesha nia ya kufadhili ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sehemu ya Kahama – Bulyanhulu – Geita yenye urefu wa kilometa 120.2,” amesema.
Amesema, wakati ujenzi wa kiwango cha lami ukisubiri upatikanaji wa fedha, wizara hiyo inaendelea kuihudumia barabara hiyo ili iweze kupitika majira yote ya mwaka, ambapo katika mwaka wa fedha 2020/21, jumla ya Shi. 872.966 milioni zimetengwa kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hiyo.
“Ninapenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kuwa, ili ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ufanyike, hatua mbalimbali hufuatwa ambazo ni pamoja na upembuzi yakinifu, usanifu wa kina.
“Utayarishaji wa nyaraka za zabuni na taratibu za ununuzi za kumpata mkandarasi wa ujenzi. Hivyo, kukamilika kwa hatua tajwa, maana yake ni kuanza kwa mradi husika,” amesema.
Leave a comment