UJENZI wa Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma nchini Tanzania umefikia asilimia 91 na utakamilika Mei 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamesemwa jana Jumapili, tarehe 16 Januari 2022 na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Mhandisi Daudi Kondoro aliyesema, ujenzi huo utakamilika na kukabidhiwa Mei kama inavyotarajiwa kwani sasa uko katika hatua za mwisho za ukamilishaji.
Mhandisi Kandoro alikuwa akitoa maelezo kwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ambaye alikagua ujenzi huo na kuonesha kuridhishwa na kasi ya ujenzi na ubora wa majengo hayo huku akimtaka mkandarasi ahakikishe mradi huo unakamilika Mei 2022.
Majaliwa alisisitiza wakandarasi kuhakikisha wanakamilisha mradi huo kwa wakati na kuwapongeza wote wanaohusika na ujenzi.
“Tunataka kumuwezesha Mheshimiwa Rais kufanya kazi katika eneo lake maalum na afanye kazi katika mazingira mazuri na kwa ufanisi,” alisema Majaliwa.
“Nimefurahishwa na taarifa kwamba ujenzi huu umefikia asilimia 91 na hatua iliyobaki hizi asilimia tisa ni kazi ndogondogo kama uwekaji wa milango, njia za mifumo ya hewa na umeme na zote zinaenda vizuri.”
Waziri Mkuu alisema Rais Samia Suluhu Hassan pia anatarajia kuona ujenzi huo unakamilika kwa wakati.
Waziri Mkuu alilipongeza Jeshi la Wananchi wa Tanzania kwa kutekeleza ujenzi huo kwa ufanisi. “Ramani iliyoko hapa iko sawasawa na jengo la Ikulu lililoko Dar es Salaam, Wakandarasi wetu mmefanya kazi kubwa sana, Hii imedhihirisha kuwa nchi yetu ina wataalam wa kutosha kujenga aina yoyote ya majengo.”
Leave a comment