WAZIRI wa Nishati nchini Tanzania, Dk. Medard Kalemani, amesema takribani Sh. 28 bilioni, zimetengwa kwa ajili ya kulipa fidia wananchi 3,832, ambao maeneo yao yatachukuliwa kwa ajili ya utekezaji Mradi wa Bomba la Mafuta Ghafi la Afrika Mashariki (EACOP). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Dk. Kalemani amesema hayo leo Alhamisi tarehe 20 Mei 2021, katika hafla yua utiaji saini mkataba wa utekelezaji mradi huo wa boda la mafuta Hoima nchini Uganda- Tanga, Tanzania, iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni.
Amesema fedha hizo zitatolewa na Kampuni ya EACOP.
Amesema, ardhi ya wananchi 391 yenye ukubwa wa ekari 325, itachukuliwa kwa ajili ya ujenzi wa kambi na ardhi ya wananchi 3,441 yenye ukubwa wa ekari 9,122, itachukuliwa na wawekezaji hao kwa ajili ya kupitisha bomba.
“Kuhusu utaratibu wa kupata ardhi fidia, imepatikana, eneo la makambi zitachukuliwa ekari 325 kutoka kwa wananchi 391, na eneo la kupitisha bomba zitachukuliwa hekari 9,122 kutoka kwa wananchi 3,441, ujumla fidia imeenza kuandaliwa takribani Sh.28 bilioni,” amesema Kalemani.
Dk. Kalemani amesema, mradi huo utapita katika vitongoji 527 kwenye wilaya 24 katika mikoa nane, Kagera, Geita, Tabora, Dodoma, Singida, Manyara na Tanga.
Mradi huo unatarajiwa kutekelezwa kwa muda wa miaka mitatu (2021 hadi 2024).
Leave a comment