SHIRIKA lisilo la kiserikali linalotoa msaada wa kisheria (Legal Services Facility-LSF), limeiomba Serikali ya Tanzania, kuondoa sheria zinazokandamiza uhuru wa vyombo vya habari. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatatu tarehe 3 Mei 2021 na Afisa Mtendaji Mkuu wa LSF, Lulu Ng’wanakilala wakati akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Vyombo vya Habari zilizofanyika kitaifa Jijini Arusha.
“Tunajua bado kuna sheria zinazoonekana zinahitaji marekebisho kwa ajili ya ustawi wa vyombo vya habari. Ni muda muafaka sasa kwa serikali kutazama namna bora ya kuziboresha sheria hizi ili kujenga mazingira rafiki ya waandishi,” amesema Ng’wanakilala.
Ng’wanalala amesema, vyombo vya habari vinasaidia katika kutokomeza vitendo vya ukatili wa kijinsia.
“Vyombo vya habari vimesaidia kukemea vitendo vya ukatili wa kijnisia, ukandamizwaji wa wanawake na watoto wa kike lakini kukemea vitendo vya uvunjifu wa amani,” amesema Ng’wanakilala.
Mtendaji huyo wa LSF amesema, vyombo vya habari vina mchango mkubwa katika kuleta maendeleo ya nchi.
“Sote tunatambua kuwa vyombo vya habari vimekuwa ni mhimili mkubwa katika maendeleo popote pale duniani, kwa kutoa taarifa zinazolenga kujenga misingi ya uwajibikaji katika jamii kwa kuhabarisha, kuelimisha na kuburudisha,” amesema Ng’wanakilala na kuongeza:
“Wakati mwingine vyombo vya habari husimamia mamlaka za kiserikali na kuibua masuala mbalimbali yaliyojificha kwa maslahi mapana ya wananchi wa kawaida.”
Leave a comment