MBUNGE wa Mafinga Mjini (CCM), Cosato Chumi, ameitaka Ofisi ya Rais, Tawaza za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) Tanzania kueleza ni lini itamaliza tatizo la walimu wa sayansi na hesabu mkoani Iringa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea)
Chumi amehoji leo Alhamisi tarehe 28 Mei, 2020 bungeni alipouliza swali kwa njia ya mtandao na kujibiwa kwa njia hiyohiyo na waziri wa elimu, sayansi na teknolojia.
“Serikali ilipopanga walimu wa sayansi na hesabu katika Halmashauri za Miji, Halmashauri ya Mafinga Mjini (mkoani Iringa) haikupata mwalimu hata mmoja. Je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa sayansi na hesabu Mafinga Mjini,” ameuliza Chumi.
Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Tamisemi amesema, kuanzia mwaka wa fedha 2015/16 hadi Februari, 2020 Serikali imeajiri watumishi 7,218 wa shule za Sekondari wakiwemo walimu 6,921 na mafundi sanifu wa maabara 297 ambapo Halmashauri ya Mji Mafinga imepatiwa walimu 25.
“Serikali itaendelea kuajiri na kuwapanga walimu wa sayansi na mafundi sanifu maabara kadri ya upatikanaji wa fedha,” amesema waziri.
Leave a comment