CHAMA cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania, kimeielekeza Serikali kuweka mikakati itakayomaliza changamoto ya uhaba wa sukari nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Pwani … (endelea).
Maelekezo hayo yametolewa leo Jumamosi tarehe 23 Mei 2020, na Dk. Bashiru Ally, Katibu Mkuu wa CCM, wakati akikagua ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere, wilayani Kibaha mkoa wa Pwani.
Dk. Bashiru amemwelekeza Japhet Hasunga, Waziri wa Kilimo na Innocent Bashungwa, Waziri wa Viwanda na Biashara, kuchapa kazi, ili Tanzania isiendelee kuwa tegemezi katika bidhaa ya sukari.
Mtendaji mkuu huyo wa chama tawala amesema, Tanzania haikupaswa kuwa tegemezi katika suala la sukari, kwa kuwa ina miundombinu ya kutosha, ambayo itachochea shughuli za uzalishaji wa malighafi za kutengeneza sukari na viwandani.
Wakati huo huo, Dk. Bashiru amesema katika Ilani ya Uchaguzi wa mwaka 2020/25 ya CCM, inayotengenezwa hivi sasa, chama hicho kimezingatia uboreshwaji wa sekta ya kilimo na viwanda.
“Sasa ni lazima tupange kujitosheleza kwa sukari na mengine, ili na sisi tuwauzie wenye uhitaji. Na katika ilani tunayoitengeneza tumeweka uhusiano mkubwa wa kilimo na viwanda. Sasa tunataka mawaziri wa viwanda na biashara wachape kazi zaidi kuliko sekta zingine zote,” amesema Dk. Bashiru.
Dk. Bashiru amesema, Tanzania inapaswa kuboresha zaidi sekta ya kilimo na viwanda, ili iachane na utegemezi wa bidhaa za mazao kutoka nje ya nchi.
“Kwa sababu tayari tumeshaweka miundominu thabiti ya umeme, reli, barabara, elimu, hatuna tena sababu ya kuwa wategemezi kutoka viwanda vya nje. Kwa sababu kujitegemea kiuchumi kunategemea sana namna sekta za viwanda na kilimo zinavyoshirikiana,” amesema Dk. Bashiru.
Maagizo hayo ya Dk. Bashiru kuhusu sukari yanatokana na changamoto iliyopo sasa ya uhaba wa sukari kwa baadhi ya maeneno nchini ambapo ilishuhudia sukari ikipanda kwa kilo hadi kufikia Sh.4,000 hadi Sh5.5000.
Leave a comment