UCHIMBAJI wa kwanza wa mafuta kibiashara nchini Uganda umeanza wiki hii, ikiwa ni sehemu ya mradi wa dola za Marekani bilioni 10 wa kuendeleza vinu vya mafuta nchini humo na bomba lenye utata linalokwenda mpaka pwani ya Tanzania. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Serikali inasema imeshughulikia masuala yanayoleta mashaka kuhusu athari za miradi ya mafuta kwa mazingira na kuwahamisha watu.
Uganda imeanza safari yake ya uzalishaji mafuta kwa kuwasha mtambo wa kuchimba visima juzi tarehe 24 Januari 2023 katika kitalu cha mafuta cha Kingfisher kusini magharibi mwa wilaya ya Kikuube.
Kitalu hicho kinachoendeshwa na Shirika la Serikali ya China ya National Offshore Oil Corporation (CNOOC), kimegharimu takriban dola bilioni mbili ikiwa ni sehemu ya mradi wa dola bilioni 10 wa kuendeleza hifadhi ya mafuta ya Uganda na kujenga bomba hadi Tanzania.
Mkuu wa Mamlaka ya mafuta ya Uganda, Ernest Rubondo amesema watachimba visima 31 kwenye kitalu cha mafuta cha Kingfisher na 10 kati ya hivyo vitakuwa kabla ya kuanza uzalishaji katika kipindi cha miaka miwili.
“Kitalu cha mafuta cha Kingfisher kinakadiriwa kuwa na jumla ya mapipa ya mafuta milioni 560. Kati ya hayo, milioni 190 yanatarajiwa kuzalishwa kwa kipindi cha miaka kati ya 20 hadi 25. Kitalu hiki cha mafuta kinatarajiwa kuwa na kiwango cha juu cha uzalishaji wa mapipa 40,000 kwa siku, kwa miaka mitano.”
Kitalu cha mafuta cha Tilenga nchini Uganda, kinachoendeshwa na kampuni ya Total Energies ya Ufaransa, kinatarajiwa kuzalisha mapipa 190,000 kwa siku.
Uganda pia mwaka huu inaanza ujenzi wa bomba lenye urefu wa kilomita 1,400 hadi bandari ya Tanga, Tanzania, ambapo mafuta hayo yatasafirishwa kwenye masoko ya kimataifa.
Leave a comment