BAADHI ya Viongozi wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (DARUSO), wamesimamishwa masomo, kwa kosa la kutoa tamko la kuishinikiza changamoto ya ucheleweshaji mikopo, kutatuliwa ndani ya saa 72. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hatua hiyo imechukuliwa na Uongozi wa UDSM, ikiwa ni itekelezaji wa agizo la Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, la kuwachukulia hatua viongozi wa DARUSO waliotoa tamko hilo.
Miongoni mwa wanaodaiwa kusimamishwa masomo ni Hamis Mussa, Rais wa DARUSO.
MwanaHALISI ONLINE ilimtafuta Mussa kwa njia ya simu, kuzungumza nae kuhusu suala hilo, leo tarehe 18 Desemba 2019, ambapo amethibitisha kuwa ni kweli wamesimamishwa masomo.
Mtandao huu ulipotaka taarifa zaidi kuhusu suala hilo, Mussa alisema hawezi kuzungumza zaidi kwa kuwa alikuwa sehemu mbaya. Na kushauri atafutwe baadae.
“Siko sehemu nzuri, ila huo ndio ukweli. Kwa sasa siwezi kuzungumza zaidi, tutazungumza baadae. Nitafute baadae,” amesisitiza Mussa.
Sakata hilo lilianza kuibuka Jumapili ya tarehe 15 Desemba mwaka huu, baada ya DARUSO kutoa saa 72 kwa Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kutoa fedha za mikopo, kwa wanafunzi waliokosa.
Pamoja na kurudisha fedha ilizokata kwa baadhi ya wanafunzi.
Baada ya tamko hilo, Wizara ya Elimu iliagiza HESLB kukutana na uongozi wa UDSM pamoja na wawakilishi wa DARUSO, kwa ajili ya kutatua changamoto zilizopo.
Katika kikao hicho kilichofanyika Jumatatu ya tarehe 16 Desemba 2019, HESLB iliahidi kuanza kutoa fedha za mikopo tarehe 18 Desemba mwaka huu.
Lakini baadae Prof. Ndalichako aliagiza waliotoa tamko la kuishinikiza HESLB kutatua changamoto za mikopo, kuchukuliwa hatua.
Leave a comment