VYAMA visivyokuwa na uwakilishi bungeni, TLP, UMD na DP, kesho tarehe 17 Novemba 2019 vitaanza kufanya kampeni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Hayo wamesema viongozi wa vyama hivyo, katika nyakati tofauti leo tarehe 16 Novemba, 2019, wakati wakizungumza na mtandao wa MwanaHALISI ONLINE, kwa njia ya simu.
Augustino Mrema, Mwenyekiti wa Chama cha TLP, amesema atazindua kampeni za chama hicho, katika Kijiji cha Kiraracha, Marangu Magharibi, mkoani Kilimanjaro.
“Mimi kesho nitazindua kampeni za chama changu kwenye kijiji changu cha Kiraracha, Marangu Magharibi, jimbo la Vunjo mkoani Kilimanjaro,” amesema Mrema.
Abdul Mluya, Katibu Mkuu wa chama cha DP, amesema chama chake kitazindua kampeni za uchaguzi huo, katika wilayani Buhingwe, mkoani Kigoma.
Hata hivyo, Mluya amedai kuwa, wagombea wake wengi wanashawishiwa na baadhi ya wananchi kujitoa katika uchaguzi huo.
Kamana Mrenda, Mwenyekiti wa Chama cha UMD, ameeleza kuwa, wamejipanga vyema kufanya kampeni katika maeneo waliyosimamisha wagombea. Na kwamba, chama chake kitazindua katika wilayani Kabondo mkoani Kigoma.
Kampeni za uchaguzi huo zinatarajia kuanza kesho, na kumalizika tarehe 23 Novemba mwaka huu. Kisha uchaguzi utafanyika tarehe 24 Nove,ba 2019.
Leave a comment