RAIS John Magufuli ameonya viongozi wa mikoa na wilaya, watakayofanya vibaya kwenye zoezi la uandikishaji wapiga kura, katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa utakaofanyika tarehe 24 Novemba, 2019. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Rais Magufuli ametoa onyo hilo wakati akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa safari za ndege za Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) iliyofanyika leo tarehe 12 Oktoba 2019, kwenye Uwanja wa Ndege wa Mpanda, mkoani Katavi.
Rais Magufuli ameeleza kuwa, viongozi wa mikoa itakayofanya vibaya katika zoezi hilo, atawachukulia hatua, kwa kushindwa kuhamasisha wananchi kujiandikisha katika daftari la wapiga kura.
“Nasubiri zoezi limazike, na kwa viongozi ambao mikoa na wilaya zao zitafanya vibaya. Najua Watanzania hawatanilaumu kwa hatua nitakazochukua kwa viongozi hao,” amesema Rais Magufuli.
Wakati Rais Magufuli akitoa onyo hilo, Zitto Kabwe, Kiongozi Mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo amesema suluhu ya tatizo hilo siyo vitisho, bali ni ushawishi utakaohamasisha wananchi kujiandikisha kwa ajili ya kupiga kura.
Zitto ameeleza kuwa, wananchi wengi wanasita kujiandikisha kutokana na kukosa imani juu ya masuala ya siasa.
“Ni kweli hali ya uandikishaji siyo nzuri, wananchi wengi wamegoma kujiandikisha. Jawabu siyo vitisho kwani sheria zetu hazilazimishi watu kujiandikisha. Jawabu imani ya watu kwenye Siasa. Imani hujengwa kwa ushawishi sio vitisho. Anachofanya hapa Rais Magufuli ni hatari sana,” ameandika Zitto katika ukurasa wake wa Twitter.
Zoezi la uandikishaji wapiga kura kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa limeanza tarehe 8 Oktoba na linatarajia kumalizika Oktoba 14 mwaka huu.
Leave a comment