WARAKA wenye kurasa 18 kuhusu uchaguzi mkuu, umetolewa na Jumuiya na Taasisi za Kiislam ukisisitiza mambo muhimu ikiwemo Tume Huru ya Uchaguzi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kwenye waraka huo uliosomwa na Sheikh Ponda Issa Ponda, katibu wa jumuiya hiyo leo tarehe 9 Julai 2020 jijini Dar es Salaam, umeitaka serikali kuhakikisha uchaguzi mkuu wa mwaka huu unakuwa huru na haki pia umuhimu wa kuwa na Katiba Mpya.
“Kwa hakika maelezo yetu ya nini tunataka kwa taifa letu katika uchaguzi huu, yangekuwa na maana sana kama Taifa lingekuwa na Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Tume Huru ya Uchaguzi, vinavyotokana na Wananchi wenyewe,” amesema Sheikh Ponda.
Soma zaidi:-
-
Mnyika: Tunataka tume huru, nguvu ya umma haijawahi kushindwa
-
Joto la tume huru lapanda
-
Prof. Safari: Bila tume huru, ni vigumu kuingia Ikulu
Hata hivyo, Sheikh Ponda amesema kama Tume Huru ya Uchaguzi haitapatikana na kwa kuwa, serikali imeahidi kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na wa haki, inatakiwa ifanyie maboresho kanuni za uchaguzi na za uendeshaji zoezi la uchaguzi.
Amesema, ni matamano ya Waislamu kuona Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), zitunge kanuni zitakazoendana na wakati uliopo.
“Mamlaka za Uchaguzi Tanzania Bara na Visiwani NEC na ZEC, zione dharua iliyopo ziitishe mabaraza ya kutunga Kanuni za Uchaguzi.
“Katika hatua hiyo muhimu Serikali izishirikishe makundi muhimu vikiwemo vyama vya Siasa. Huo pia ni wito wa Watanzania mbali mbali wamekuwa wakipendekeza maboresho ya kanuni katika kipindi hiki cha mpito,” amesema Sheikh Ponda.
Katibu huyo amesema, katika maboresho hayo, kanuni za uchaguzi ziruhusu vyama vya siasa kupata nakala ya Daftari la Wapiga Kura kabla ya uchaguzi huo.
“Kanuni itamke na kuweka msisitizo wa hatuwa za kisheria kuwa viongozi wa Serikali kama Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Watumishi wa Umma wasitumike kisiasa katika kipindi hiki cha kuelekea Uchaguzi Mkuu, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi,” amesema Sheikh Ponda.
Amsema, “kanuni itamke Mashirika na Taasisi za Umma hawaruhusiwi kufanya kampeni ya mgombea yoyote au chama chochote cha siasa.
“Kanuni itamke Kura zitapigwa na kuhesabiwe katika kituo husika cha kupigia kura. Itamke wazi baada ya kuhesabiwa hazitahamishwa katika kituo hicho na kupelekwa katika kituo kingine chochote kwaajili ya kuhesabiwa upya,” amesema.
Amesisitiza kwamba, iwapo mapendekezo yao yatafanyiwa kazi, yatapunguza athari za kutokuwepo kwa Tume Huru ya Uchaguzi.
“Mapendekezo hayo yatapunguza kwa kiasi kikubwa ombwe la kukosekana Tume Huru ya Uchaguzi, na yanaleta matumaini ya Uchaguzi Huru na wa Haki katika kipindi hiki cha mpito cha madai ya wananchi ya Tume Huru,” amesema Sheikh Ponda.
Leave a comment