WAKENYA watajua rais wao mpya wakati wowote kuanzia leo wakati Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Wafula Chebukati akiwa amebakisha siku moja ya kesho Jumanne pekee kama siku anayopaswa kutangaza mshindi wa kura ya urais iliyofanyika Agosti 9, 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Kwa mujibu wa Katiba, Chebukati ambaye ni msamizi wa uchaguzi wa urais, ana siku saba tangu tarehe ya uchaguzi, kutangaza matokeo ya kura ya urais, siku ambazo zinakamilika kesho Jumanne.
Ibara ya 138(10) ya katiba ya Kenya inasema kwamba tume ya uchaguzi ina siku saba kutoka tarehe ya uchaguzi kutangaza mshindi wa kura ya urais.
“Ndani ya siku saba baada ya uchaguzi wa urais, mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka aya (a) kutangaza matokeo ya uchaguzi; na (b) kuwasilisha ilani ya maandishi ya matokeo kwa Jaji Mkuu na rais aliye mamlakani,” inaeleza ibara hiyo.
Uchaguzi mkuu ulifanyika Agosti 9, 2022 na vituo vingi vilifungwa kabla ya saa 11 jioni siku hiyo huku vichache vikichelewa kufungwa kwa kuwa vilifunguliwa kuchelewa.
Ujumuishaji na uthibitishaji wa matokeo kutoka maeneo-bunge yote 290 umekuwa ukiendelea kwa mwendo wa taratibu katika ukumbi wa Bomas of Kenya, Nairobi huku maafisa wa IEBC wakikagua na kutathmini fomu 34A kutoka katika zaidi ya vituo 46,000 vya kupigia kura kote nchini.
Hata hivyo, kulingana na katiba, mchakato huo ni lazima ukamilike kufikia leo Jumatatu usiku wa manane na mshindi kutangazwa ili kuepusha nchi dhidi ya mzozo wa kikatiba.
Leave a comment