TUME ya Uchaguzi Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), imetangaza kwamba uchaguzi mkuu nchini humo sasa utafanyika Desemba 2018.
Hata hivyo, upinzani haujafurahishwa na hatua hiyo ambao umetaka Rais Joseph Kabila aondoke madarakani kwa sasa.
Awali uchaguzi huo ulipangwa kufanyika mwaka huu chini ya makubaliano yaliyoafikiwa mwaka jana, lakini tume ya uchaguzi imechelewa kuuandaa.
Lakini sasa tume hiyo imetangaza kwamba uchaguzi wa rais, wabunge na viongozi wa serikali za majimbo utafanyika mnamo 23 Desemba, 2018.
Upinzani umepinga tarehe hiyo na kusema haikubaliki huku ukisisitiza kwamba kwamba ni sharti Rais Kabila aonondoke madarakani kufikia mwisho wa mwaka huu.
“Tunaikataa kalenda iliyotolewa ya uchaguzi…tunachokitaka kwa sasa hivi ni Kabila kuondoka madarakani kufikia 31 Desemba, 2017,” alisema Augustin Kabuya, msemaji wa chama kikuu cha upinzani cha Union for Democracy and Social Progress (UDPS).
Ofisa wa tume ya uchaguzi, Jean-Pierre Kalamba amesema matokeo ya awali katika uchaguzi huo yatatangazwa katika kipindi cha wiki moja baada ya upigaji kura kufanyika, mnamo tarehe 30 Desemba, lakini matokeo kamili yatatangazwa tarehe 9 januari, 2019.
Rais mpya anatarajiwa kuapishwa 12 Januari, 2019. Kiongozi wa upinzani Moise Katumbi amepuuza mpango huo tume ya uchaguzi .
“Utawala huu dhalimu unataka kuendeleza ukosefu wa uthabiti na dhiki dhidi ya wananchi,” Katumbi amesema.
“Hatutakubali kalenda hii. Kabila sharti aondoke,” aliandika kwenye Twitter.
Hali ya wasiwasi imekuwepo nchini humo tangu Kabila alipokataa kuondoka madarakani mwishoni mwa mwaka jana baada ya kumalizika kwa muhula wake wa pili na wa mwisho.
Tume ya uchaguzi imesema moja ya sababu iliyosababisha kushindwa kuandaa uchaguzu kwa wakati ni kutokana na matatizo ya kuandaa sajili ya wapiga kura, hasa eneo lenye misukosuko la Kasai katikati mwa nchi hiyo.
Leave a comment