KUELEKEA Uchaguzi Mkuu Oktoba 2020, Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC) umesema, utaendesha mafunzo maalum kwa waandishi wa habari ya namna watakavyofanya kazi zao kwa usalama pamoja na kuwajengea uwezo mawakili wanaotetea haki za binadamu. Anaandika Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamesemwa na Mratibu wa mtandao huo, Onesmo Olengurumwa wakati akisaini mkataba wa Dola za Kimarekani 120,000 ambazo ni sawa na Sh. 277 milioni na Shirika la wafadhili la Initiative for Eastern Africa (OSIEA) kwa ajili ya kuendesha mafunzo hayo.
Olengurumwa amesema, mafunzo hayo yana lengo la ushirikiano na Serikali, Mahakama na kuweka mazingira mazuri ya ufanyaji kazi kwa watetezi wa haki za binadamu.
Amesema, mkataba huo ni wa kipindi cha mwaka mmoja ambao ni kama nyongeza kwakuwa shirika hilo ni wadau wakwanza waliowapa fedha za uanzilishi wa taasisi tangu 2012 hadi leo wamekuwa wakifanya kazi pamoja.
“Hizi ni kama fedha za nyongeza ya fedha ambazo tumeendelea kuzipokea kutoka kwao kwa miaka yote kila mwaka, kwa utaratibu tuliouzoea tunapopata fursa, tunaposaini mkataba ni vyema tukatoa taarifa kwa wadau wenzetu juu ya washirika wetu tunavyoshirikiana nao,” amesema.
Amesema shughuli za watetezi wa haki za binadamu zinakuwa katika mazingira magumu hasa katika kipindi cha uchaguzi hivyo fedha hizo zitasaidia kuboresha shughuli za kuwajengea uwezo watetezi wa haki za binadamu katika masuala ya usalama na utetezi.
Pia, kusimamia sheria mbalimbali na kuwagusa mawakili wanaotetea haki za binadamu katika maeneo ya kusimamia kesi za uchaguzi pamoja na watetezi waangalizi wa uchaguzi.
Leave a comment