CHAMA cha Sauti ya Umma (Sau) nchini Tanzania, kimewapitisha wagombea wa urais wa Tanzania na Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkutano Mkuu wa chama hicho umefanyika leo Jumamosi tarehe 25 Julai 2020 jijini Dar es Salaam ambapo Muttamwega Mgaywa amepitishwa kugombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mgombea mwenza atakuwa, Satia Musa Sebwa huku mgombea urais wa Zanzibar ni Issa Mohamed Nzonga.
Katibu Mkuu wa SAU, Majalio Kyara amesema, wagombea hao wamepigiwa kura kupitia mkutano mkuu wa chama baada ya kamati kuu ya chama hicho kuwajadili na kuyapendekeza majina mawili yapelekwe kwenye mkutano mkuu ili wapigiwe kura
“Awali, waliotia nia ya kugombea nafasi ya urais upande wa Tanzania majina yalikuwa matano lakini waliochukua fomu na kurudisha walikuwa wawili nikiwemo mimi (Kyara) pamoja na Mgaywa lakini niliamia kujiondoa ili aendelee na mchakato huu,” Kyara amesema.
Mara baada ya kutangazwa kuwa mgombea, Mgaywa amesema, nia yake ni kukijenga chama na siyo kuwa mpinzani wa maendeleo ambapo mawazo yao kwenda Ikuru.
Amesema, anataka kuijenga SAU kiwe chama cha kuleta maendeleo kama anavyofanya Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli alivyoiletea nchi maendeleo.
Kwa upande wake, Nzonga amesema, anagombea nafasi hiyo kwa mara ya pili kupitia chama hicho hivyo aliwaomba wananchi watakapomchagua atafuata nyendo za Rais Magufuli kwa kuwa anafanya vizuri katika maendeleo.
“Tumeona Zanzibar Rais wa awamu ya saba na Rais Magufuli wamefanya vizuri katika maendeleo hivyo na mimi nitafuata nyendo zao,” amesema
Awali, Msajili Msaidizi wa vyama vya siasa, Sisty Nyahoza alisema alihudhuria mkutano huo kuangalia uchaguzi wa wagombea ambao umekwenda vizuri.
Amesema suala la rushwa likisimamiwa vizuri na vyama husika kwenye mchakato wa nafasi za ubunge, udiwani na urais watakaoenda tofauti wawachukulie hatua.
Leave a comment