WAKATI Tume ya Taifa ya Uchaguzi Tanzania (NEC), ikisema Chama upinzani cha Wananchi (CUF), kitashiriki uchaguzi mdogo wa Jimbo la Konde, Zanzibar, chama hicho kimesema hakitashiriki. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya CUF kutoshiriki uchaguzi huo mdogo, imetolewa leo Jumapili, tarehe 19 Septemba 2021 na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma, Mhandisi Mohammed Ngulangwa, akizungumza na MwanaHALISI Online.
“CUF hatushiriki uchaguzi wa Konde, kama kutakuwa na yeyote atakayejitokeza kugombea mshangae inakuwaje wanajitokeza watu wanafakiwa kugombea hata kama hawajachaguliwa na kudhaminiwa na chama,” amesema Ngulangwa.
Taarifa hiyo ya CUF imekuja saa chache baada ya Mkurugenzi wa Uchaguzi NEC, Dk. Wilson Mahera, kusema vyama vinne vitashiriki uchaguzi mdogo wa Konde, ikiwemo chama hicho, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na ACT-Wazalendo.
Hata hivyo, Mkurugenzi huyo wa Habari CUF amesema, chama hicho hakijabadili msimamo wake wa kutoshiriki uchaguzi hadi tume huru ya uchaguzi na katiba mpya vitakapopatikana.
NEC iliitisha uchaguzi mdogo katika Jimbo la Konde utakaofanyika tarehe 9 Oktoba mwaka huu, baada ya mbunge wake mteule kupitia CCM, Sheha Mpemba Faki, kujiuzulu kabla ya kuapishwa kwa sababu za kifamilia.
Awali, jimbo hilo lilikuwa wazi baada ya aliyekuwa mbunge wake kupitia ACT-Wazalendo, Khatib Said Haji, kufariki dunia tarehe 20 Mei 2021.
CUF kilitoa msimamo huo baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2020 kufanyika, ambao kilitangaza kutotambua matokeo yake yaliyokipa ushindi wa kishindo chama tawala cha CCM, katika kiti cha urais, ubunge na udiwani.
CUF kilitangaza kutotambua matokeo hayo kikidai kwamba mchakato wa uchaguzi huo haukuwa huru na wa haki, tuhuma zilizopingwa na NEC, iliyosema imeendesha uchaguzi kwa misingi ya haki, uhuru na kwa kufuata matakwa ya sheria
Leave a comment