KIKOSI kazi cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya siasa za vyama vingi imesema ubinafsi na kutoaminiana ni miongoni mwa changamoto zinazokwamisha maridhiano ya kisiasa nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yameelezwa leo Jumatatu tarehe 21 Machi 2022 na Mwenyekiti wa Kikosi kazi, Profesa Rwekaza Mukandara wakati akiwasilisha taarifa ya awali ya utendaji kazi wa kikosi kazi hicho kwa Rais Samia Suluhu Hassan Ikulu.
“Kutoaminiana kwa wanasiasa kunafanya mazungumzo na kufikia maridhiano kuwa ngumu katika nyakati tofauti…ubinafsi unaofanywa na baadhi ya wanachama wa vyama vya siasa kujali zaidi maslahi ya vyama vyao kuliko maslahi ya Taifa,” ameeleza Prof. Mukandara.
Mukandara ametaja sababu zingine kuwa ni kutokuwa na utaratibu rasmi wa kuwezesha maridhiriano ya vyama vya siasa pindi unapotokea mgogoro, vyama vya siasa na taasisi nyingine zinazihusika na masuala ya siasa na kidemokrasia kutokuwa na utaratibu wa kuelezana, kuelimishana na kujadiliana.
Pia ametaja sababu nyingine kuwa ni baraza la vyama vya siasa kutotekeleza majukumu yake ipasavyo mfano kutofanya vikao vya mara kwa mara.
Ili kuondokana na mkwamo huo Kikosi kazi hicho kimependekeza kuimarishwa utamaduni wa kufanya mazunguzmo na kufikia maridhiano ya shughuli za kisiasa kuimarisha uzalendo wa taifa katika kufanya shughuli za siasa, kuboresha utendaji wa baraza la vyama vya siasa, kupendekeza namna bora ya kujenga utamaduini wa kuaminiana kati ya Serikali na vyama vya siasa, wanasiasa na taasisi zingine na kuhakikisha demokrasia ndiyo mchezo pekee unaotawala nchini.
Leave a comment