MWITIKIO hafifu wa watu kujitokeza katika uandikishaji kwa ajili ya kupiga kura, kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa baadaye mwaka huu, umehusishwa na misimamo ya Rais John Mafufuli. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Miongoni mwa lawama hizo ni kuzuia mikutano ya hadhara, jambo ambalo linadaiwa kusababisha wananchi kukosa hamasa ya kwenda kujiandikisha.
Mneke Jaffar, Mkurugenzi Mipango na Uchaguzi Chama cha Wananchi (CUF) amesema, miaka ya nyuma wananchi walikuwa wakisukumwa kujiandikisha kutokana na ushawishi wanaoupata kutoka kwenye mikutano ya kisiasa.
Mikutano ya kisiasa imepigwa marufuku kwa wanasiasa wasio kwenye maeneo yao husika, kwenda kufanya mikutano ya hadhara. Msimamo huo wa serikali ya awamu ya tano umekuwa ukilalamikiwa.
Jaffar amesema, chaguzi za serikali za mitaa zilizopita akitaja mwaka 2004, 2009 na 2014 zilikuwa na hamasa kwa kuwa, wananchi waliahamasishwa kwenye mikutano ya hadhara.
“Lakini pia wananchi wanaonekana kuchoshwa na kukata tamaa baada ya kuona wanaopata kura chache, ndio wanatangazwa kuwa washindi.
“Wananchi wana wasiwasi kuhusu utayari wa serikali ya CCM kushuhudia kampeni za uchaguzi zikifanyika, wengi wanaamini kuwa CCM imenogewa kuwa msema pweke’ hivyo kujitangaza washindi hata kama hatojashinda,” amesema.
Jaffar anaamini, wananchi wanaopigia wapinzani wamefadhaishwa na mchezo mchafu kwa wabunge na madiwani kujipeleka CCM wakidai kumuunga mkono Rais Magufuli.
“Tungependa serikali kupitia TAMISEMI, izuie vitendo vya wasimamizi kuhamisha vituo na kwenda majumbani kuandikisha watu kiholela kama ilivyoripotiwa Tanga na Mtwara.
“Serikali iwaondolee hofu wananchi na kutoa tamko la rasmi vyama vya siasa kufanya mikutano ya hadhara, ili kuhamasisha wananchi kujiandikisha na kuzungumzia masuala yanayohusu nchi yao kama Katiba ya Nchi inavyotaka,” amesema.
Leave a comment