Saturday , 3 June 2023
Home Gazeti Habari za Siasa Uamuzi juu ya wakurugenzi kusimamia uchaguzi 13 Juni
Habari za SiasaTangulizi

Uamuzi juu ya wakurugenzi kusimamia uchaguzi 13 Juni

Sanduku la kura
Spread the love

 

MAHAKAMA ya Afrika ya Haki za Binadamu (ACHPR), imepanga kutoa uamuzi wa shauri la madai lililofunguliwa na Bob Chacha Wangwe, dhidi ya Serikali ya Tanzania, kupinga wakurugenzi wa halmashauri kusimamia uchaguzi, Juni mwaka huu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Arusha …. (endelea).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na mahakama hiyo yenye makao yake makuu jijini Arusha nchini Tanzania, shauri hilo linalosubiriwa kwa hamu na wapenda demokrasia nchini, uamuzi wake utatolewa tarehe 13 Juni mwaka huu, kuanzia saa nne asubuhi kwa saa za Afrika Mashariki.

Bob Chacha Wangwe – mwanaharakati wa haki za kikatiba nchini Tanzania – akishirikiana na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), alifungua shauri hilo katika Mahakama ya sheria ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, tarehe 8 Novemba 2020.

Mahakama ya Afrika (African Court on Human and Peoples’ Rights), ilianzishwa na nchi za Afrika ili kulinda haki za binadamu na za mataifa katika bara hilo.

Uamuzi huo ulichukuliwa na Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU), wakati huo ambapo sasa unajulikana kama Umoja wa Afrika (AU), huko Ouagadougou, Burkina Faso, Juni 1998 na kupata nguvu ya kisheria 25 Januari 2004 baada ya nchi 15 kuupitisha kwa saini.

Kwa sasa, nchi zilizoridhia mahakama hiyo, zimefikia 30; Mahakama inaundwa na mahakimu kumi na moja, wote raia wa nchi za Umoja wa Afrika.

Kesi dhidi ya serikali ya Jamhuri ya Muungano, imelenga kupinga wakurugenzi wa halmashauri, majiji na manispaa, kusimamia uchaguzi mkuu nchini Tanzania.

Waleta maombi wanalalamikia sheria inayoruhusu watumishi hao wa serikali kusimamia uchaguzi, kwa maelezo kuwa wengi wao ni makada wa chama kilichoko madarakani – Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Upinzani dhidi ya maofisa hao kusimamia chaguzi zinazofanyika Tanzania, umezidi kupamba moto katika siku za karibuni, huku madai makubwa – mbali na kuwa makada wa chama tawala, ni uteuzi wao kufanywa na rais aliyeko madarakani na ambaye naye anagombea katika uchaguzi huo; na au chama chake kinashiriki chaguzi hizo.  

Wangwe na LHRC walifungua shauri hilo, miezi mitano baada ya Mahakama ya Rufani nchini Tanzania, kutengua hukumu ya Mahakama Kuu, iliyokuwa imewazuia wakurugenzi hao, kusimamia uchaguzi kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

Mahakama Kuu ya Tanzania, chini ya jopo la majaji watatu, Dk. Atuganile Ngwala, Dk. Benhajj Masoud na Firmin Matogolo, ilifuta sheria iliyokuwa inawapa wakurugenzi hao mamlaka ya kuwa wasimamizi wa uchaguzi, tarehe 24 Mei 2019.

Kupitia maamuzi hayo, Mahakama Kuu, ilibatilisha kifungu cha 7(1) cha Sheria ya Uchaguzi kinachoipa mamlaka NEC kuwateua wakurugenzi wa majiji, manispaa na miji kuwa wasimamizi wa uchaguzi.

Aidha, Mahakama ikabatilisha kifungu cha 7(3) kinachoipa NEC mamlaka ya kuteua mtu yeyote miongoni mwa watumishi wa umma, kuwa msimamizi wa uchaguzi.

Katika hukumu hiyo, mahakama ilisema vifungu hivyo ni kinyume cha Katiba ya nchi ikibainisha kuwa wakurugenzi hao huteuliwa na Rais aliyeko madarakani ambaye hutokana na chama tawala na kwamba wengine ni wanachama wa chama cha mamlaka inayowateua, jambo ambalo huathiri utendaji wao katika kutenda haki.

Mahakama ilieleza kuwa sheria haijaweka ulinzi kwa NEC kumteua mtumishi yeyote wa umma kuhakikisha kuwa anakuwa huru katika kutekeleza majukumu yake.

Uamuzi huo ambao hata hivyo ulibatilishwa na Mahakama ya Rufani, ulitokana na kesi iliyofunguliwa na mashirika kadhaa ya wanaharakati kupitia kwa kwa mwanaharakati huyo aliyekuwa anatetewa na wakili mashuhuri nchini, Fatma Karume.

Hata hivyo, 17 Oktoba, mwaka huo huo, Mahakama ya Rufani ikatengua uamuzi huo.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari MchanganyikoTangulizi

Bosi NIC apandishwa kizimbani, akabiliwa na mashitaka 365

Spread the love  ALIYEKUWA Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Bima la Taifa...

Habari za Siasa

Lusinde: CCM hatuliachii ng’o jimbo la Moshi Mjini

Spread the loveMJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Chama cha Mapinduzi (NEC), Livingston...

Habari za SiasaTangulizi

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar: Bakharesa hajavamia shamba letu

Spread the love  IKULU Visiwani Zanzibar, imeeleza kuwa eneo la kiwanda cha...

Habari za SiasaTangulizi

Zanzibar watangaza rasmi kuwa shamba la Razaba ni mali yao

Spread the love  SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), imetangaza rasmi kwamba shamba...

error: Content is protected !!