Friday , 19 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Tusiruhusu kutawaliwa na mademagogi
Habari za SiasaTangulizi

Tusiruhusu kutawaliwa na mademagogi

Ally Hapi, Mkuu wa wilaya ya Kinondoni (kulia). Picha ndogo, Mbunge wa Kawe, Halima Mdee
Spread the love

BAADA ya mkasa uliomkuta Halima Mdee, Mbunge wa Kawe, wiki iliyopita, nimekumbuka kwa uchungu, mazungumzo yangu na waandishi wa habari tarehe 12 Februari 2017, ofisini kwangu Mwanza, anaandika Ansbert Ngurumo

Siku hiyo, niliwaeleza kuwa nchi yetu sasa inaongozwa kidemagogi. Niliomba wananchi waamke kuomba, kukemea, kushauri, kupinga na kufanya lolote ambalo litachangia kuiepusha nchi yetu na maangamizi.

Kabla ya waandishi kuniuliza demagogi ni nani, nilifafanua kwa kifupi maana yake. Na leo nitafanya hivyo.

Demagogi ni kiongozi anayejitafutia sifa kwa kuumiza wengine au kwa kutumia hofu za kijamii kujijengea umaarufu wa kisiasa.

Katika historia ya dunia, wamekuwepo mademagogi mashuhuri kadhaa, lakini wanaolaaniwa zaidi ni Huey P, Long, Joseph McCarthy, Fr. Charles Coughlin na Lewis Charles Levin.

Nilieleza kuwa udemagogi huu ulizaa pia kitu kingine kinachojulikana kama umakathi, kutokana na jina la McCarthy demagogi wa Kimarekani, aliyekuwa Seneta wa Wisconsin mwaka 1947 mpaka 1957.

Kwa muktadha wa uchambuzi huu, nitamwita Makathi. Mnamo Februari 9, 1950, Makathi alifanya kituko. Kwa kujua kwamba jamii ya Wamarekani walichukia mno Ukomunisti, aliamua kujitafutia umaarufu kwa kutuhumu raia wenzake kuwa ni wakomunisti.

Kuitwa Mkomunisti nchini Marekani kulikuwa sawa na kuitwa mhaini. Aliita vyombo vya habari, hasa televisheni, akatuhumu watu mashuhuri – wakiwamo watumishi waandamizi katika wizara nyeti ya mambo ya nje, Ikulu, Redio Sauti ya Marekani (VOA), Jeshi na kadhalika. Alisema walikuwa wanaandaa mapinduzi dhidi ya serikali.

Kutokana na hofu iliyokuwa imejengeka, na kwa kuwa haikuwahi kutokea kiongozi yeyote kufanya hivyo, na kwa kuwa waliotajwa walikuwa watu maarufu na vigogo; na kwa kuwa mkomunisti ni adui wa umma, wananchi walimuona Makathi kama shujaa wa kitaifa.

Mwanzoni waliamini alichokuwa anafanya, wakidhani kinalenga kuokoa nchi. Machoni mwa wengi, Makathi alionekana kiongozi mzalendo anayepiga vita ufisadi na uhaini.

Naye kwa kujua alicholenga kufanya, na kwa kujua wananchi hawajatambua nia yake, aliongeza kasi na mbwembwe. Hakujali katiba inasema nini kuhusu haki za hao aliokuwa anawatangaza kwenye vyombo vya habari.

Kwa kutumia vyombo vya habari, hasa katika matangazo mubashara ya televisheni, alihoji watuhumiwa, akawadhalilisha na kuwafedhehesha maofisa wa jeshi na wanasiasa.

Miongoni mwa watuhumiwa wake walikuwa wasanii mbalimbali. Baadhi yao waligoma kuhojiwa. Lakini hakuwaacha salama. Kwa kuwa watuhumiwa karibu wote walikuwa watumishi wa serikali, waliogoma kutoa ushirikiano walifukuzwa kazi.

Baadhi ya watuhumiwa, kwa sababu ya mateso, walilazimishwa kukiri hadharani, kutubu, na kutaja watu wengine kuwa ni watuhumiwa wenzao katika kashfa ya ukomunisti, ili waachiwe huru.

Hata hivyo, walijitokeza watu wachache katika jamii, wakaanza kushtuka. Wakatilia shaka mbinu alizotumia. Wakatilia shaka weledi wake wa upelelezi katika suala alilokuwa anasimamia moja kwa moja.

Miongoni mwa walioshtukia udemagogi wa Makathi ni Dwight Eisenhower, ambaye wakati utesaji huo unaendelea, alibahatika kuwa rais wa 34 wa Marekani (1953-1961).

Alichukua uamuzi mkali. Akamkana Makathi hadharani. Akamwamuru kuacha kusingizia watu na kuwafedhehesha hadharani.

Jamii nayo ikashtuka, ikaanza kumlaani Makathi na mbinu zake za kuchafua watu kwa tuhuma za kutunga. Makathi akapata anguko la kijamii na kiafya. Hakuishi miaka mingi tena, alifariki dunia akiwa amechanganyikiwa, akiwa kijana wa miaka 48.

Kutokana na jina lake, matendo na hatua za kikatili za aina hii vilizaa mtihani mpya katika lugha ya Kiingereza – McCarthyism (Umakathi).

Miaka 67 baadaye, baada ya kiongozi mmoja kijana kutembelea Marekani na kurudi, mapema mwaka huu, umakathi umeanza kuota mizizi nchini. Aliyosababishia wasanii, wanasiasa, wafanyabiashara, viongozi wa dini na wengine, na kumpa ushujaa wa muda yanafahamika. Na anakoelekea kijamii na kisiasa panaonekana.

Bahati mbaya, jamii yetu imechelewa kushtuka. Mwanzoni, baadhi ya wabunge walishtuka, lakini sauti zao hazikusikilizwa kwa kuwa wasaidizi wa kiongozi huyo walifurahia alichokuwa anafanya.

Kama ilivyokuwa Marekani, vyombo vya habari vya hapa navyo havikushtuka mapema. Viliendelea kumsaidia kusambaza ukatili huu hadi alipotenda kituko kingine dhidi ya vyombo vya habari vyenyewe.

Jeshi la Polisi, kwa bahati mbaya, nalo liliingizwa katika mkumbo; likamsaidia kukamata na kutisha raia kinyume cha utaratibu, hadi hali hiyo ilipokuja kurekebishwa baada ya watuhumiwa wanaojitambua kuchukua hatua za kisheria.

Ilichukua muda kiasi kabla ya wananchi kukumbuka kuwa demagogi huyu amezoea kupanda vyeo kwa kutendea wengine yasiyofaa.

Kwa mfano, mwaka 2013 aliteuliwa kuwa mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba baada ya kurusha matusi dhidi ya Edward Lowassa na wengine mbele ya vyombo vya habari. Mwaka 2015 aliteuliwa kuwa mkuu wa wilaya baada ya kumzaba kibao Jaji Joseph Warioba katika mdahalo wa katiba mpya.

Mwaka 2016 aliteuliwa kuwa mkuu wa mkoa baada ya kutukanana, kuzozana na kuburuzana mahakamani na Saed Kubenea, Mbunge wa Ubungo. Yumkini alikuwa anawinda nafasi kubwa zaidi kwa kituko hiki kilichoibua umakathi wake.

Bahati mbaya ninayoona ni kwamba wakuu wake na baadhi ya vijana wenzake, wamekuwa wanafikiri njia nzuri ya kujulikana na kupata sifa ni kuumiza raia. Kwanini? Wametambua kuwa mkuu wao anawafurahia pale wanapotoa matamko au wanapochukua hatua za kuumiza wale wanaodhaniwa kuwa wabaya na washindani wao.

Ndiyo maana kumekuwapo matukio ya kushangaza yanayofanywa na baadhi ya wakuu wa wilaya. Halikuwa jambo la kiungwana kwa mkuu wa wilaya ya Ubungo kuagiza polisi wamkamate na kumtia ndani kwa saa 24 Boniface Jacob, Meya wa Ubungo, eti kwa kualika viongozi wenzake wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kutembelea miradi ya maendeleo katika Manispaa anayoongoza.

Kitendo hiki, hata kama kilifurahisha wakuu wake, hakikumbakizia heshima DC huyo katika jamii ya Watanzania. Kabla siku hazijapita nyingi, mkuu wa wilaya ya Kinondoni naye akaagiza polisi wamkamate Mdee na kumweka ndani kwa saa 48.

Kisa? Alizungumza na waandishi wa habari akatetea haki ya watoto wa kike kupata elimu hata kama ikitokea wakapata mimba shuleni; akakosoa kauli ya Rais John Magufuli aliyetangulia kusema kuwa katika utawala wake watoto hao hawana haki hiyo.

Hadi naandika haya, mbunge wa Kawe alikuwa amekaa ndani kwa saa zaidi ya 70. Katika nchi ya kidemokrasia, matendo kama haya ni ya kikatili, na yanapaswa kupingwa.

Tukilea tabia hizi za kidemagogi, tutajenga jamii ambayo inazima uhuru wa wananchi kujieleza, na hivyo kuzima mawazo mbadala, ubunifu, na ndoto za maendeleo.

Tukiendekeza udemagogi huu, na tukaulea kwa woga wa jamii, tutajenga siasa za kutafutana uchawi, kuzushiana, na kuviziana. Tusipokemea mambo haya, tutajenga na kukuza hofu ya mabadiliko chanya. Zaidi, tutaharibu sifa na maisha ya watu wengine.

Nini kifanyike? Ninapendekeza. Kwanza, wananchi washtuke, waache woga, na wahimize serikali kuzingatia katiba na sheria za nchi pasina kuonea watu.

Pili, rais akubali kushauriwa. Apunguze kufoka na kutisha watu ili aweze kuletewa asiyoyajua, anayonyimwa na wasaidizi wake kwa sababu wanaogopa kupoteza madaraka.

Rais ahimize wasaidizi wake waache kujipendekeza kwake na anapogundua wanatesa watu ili wapate sifa, achukue hatua kali kama iliyochukuliwa na Rais Eisenhower niliyemtaja mapema.

Tatu, viongozi wa kiroho nao waache woga. Watambue kuwa wapo juu ya viongozi wa kisiasa. Waoneshe unabii wao kwa kukemea maovu yanayosababishwa na watawala.

Nne, wanasiasa wafanye kazi yao bila hofu, wakemee tabia hizi, hata kama kwa kufanya hivyo wanatishwa na kukamatwa. Tano, wafanyabiashara washikamane, wajitetee. Umoja wao ndiyo nguvu yao, na ndio uhai wa Watanzania.

Sita, wasanii watunge nyimbo za kuombea taifa, kuhamasisha demokrasia, ujenzi wa uchumi imara, na utetezi wa haki za raia. Huu ndio wakati wa wasanii kujitambulisha rasmi kama kioo cha jamii.

Saba, vyombo vya habari visiandike tu na kutangaza ajenda za watu kwa woga, na kulisha wananchi sumu; bali vishtuke na kuokoa taifa kwa kufanya uchambuzi wa kina wa masuala yanayoendelea.

Itakumbukwa mwaka 2011, kwa bahati mbaya, vyombo vya habari ndivyo vilikuza suala la kikombe cha Babu wa Loliondo, kwamba ana dawa ya kutibu magonjwa yote ukiwamo Ukimwi.

Miongoni mwa waliokimbilia Loliondo “kupata kikombe” ni Rais Jakaya Kikwete, mawaziri kadhaa – William Lukuvi, John Magufuli na wengine – wabunge, na wananchi wengine.

Nguvu iliyotumika kutangaza “neema” ya kikombe cha Babu, ingeweza kutumika kufanya uchambuzi wa kina kuhusu haja ya serikali kuimarisha miundombinu ya afya ili wananchi watibiwe kwa ufanisi.

Tusipofanya hivyo, tunaweza kujikuta tumejenga jamii ya walevi wa madaraka kama walivyokuwa watawala wa kale kama Lavrentiy Beria wa Urusi, Ivan The Terrible, Mfalme Commodus, Mfalme Caligula, Christian VII, Heliogabalus, Nero, Hitler, Stalin, Mussollini, Idi Amin, Mobutu Seseseko.

Hatutaki kulea watawala wa aina ya Yoweri Museveni, Paul Kagame, Paul Nkurunziza, na wenzao waliochafua sifa ya bara la Afrika kwa matendo ya kikatili yatokanayo na ulevi wa madaraka. Tukiwahi, hatutafika huko.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

KimataifaTangulizi

Mkuu wa majeshi Kenya afariki, Ruto atangaza maombolezo

Spread the loveRais wa Kenya, William Ruto ametangaza maombezo ya siku tatu...

Habari za SiasaTangulizi

Tanzania, Uturuki zanuia kukuza biashara, uwekezaji

Spread the loveSERIKALI za Tanzania na Uturuki zimekubaliana kuendeleza dhamira ya kuimarisha...

Habari za Siasa

Tume huru ya uchaguzi yatangaza ajira watendaji daftari wapiga kura

Spread the love  TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), imetangaza nafasi...

Habari za SiasaTangulizi

Chadema yatangaza ruti awamu ya pili maandamano

Spread the love  CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema awamu ya...

error: Content is protected !!