SERIKALI imeombwa kuhakikisha inaweka mipango na mikakati madhubuti ya kuwawezesha wajasiliamali wadogo nchini wanaomiliki viwanda vidogo, ili waweze kukuza mitaji yao, anaandika Moses Mseti.
Pia imeombwa kuanzisha viwanda vya kutengeneza vifungashio vya bidhaa ambavyo ni bora ili kuleta ushindani katika soko la Afrika Mashariki na kuondokana kununua vifungashio hivyo nchini ya Kenya.
Kauli hiyo imetolewa leo na wajasliamali wadogo zaidi 50 wakati walipokutanishwa kwenye mafunzo ya mbili ya usindikaji wa vyakula, ilioandaliwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) na kufanyika jijini Mwanza.
Victoria Gachocha, Anna Shayo, Augustine Kasase na Debora Mganda, wamesema kuwa wasindikaji wadogo wa bidhaa nchini wanakabiliwa na tatizo la ukosefu wa mitaji pamoja na uhaba wa viwanda vya kutengeneza vifungashio ambavyo ni bora.
Wamesema kuwa hivi sasa wanalazimika kununua vifungashio kutoka nchini Kenya kitendo ambacho kinasababisha washindwe kuleta ushindani katika soko la afrika mashariki kwa kuwa vifungashio vingi vya bidhaa zao hununua nchi jirani.
“Sisi wajasliamali wadogo wa Tanzania mitaji yetu ni midogo sana, lakini wanyarwanda wao wanasaidia sana na serikali yao kwa kupewa mitaji ya fedha, tunaiomba serikali iangalie suala hili na iweze kutusaidia na kukuza biashara zetu,” amesema Augustine Kasase.
Mwakilishi wa Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) ambaye pia ni Mratibu wa mafunzo ya wajasliamali (SME), Lazaro Mwambole, amesema kuwa asilimia 75 ya vyakula nchini vinatoka kwa wajasliamali wadogo hivyo ni lazima wapewe elimu ya usindikaji wa bidhaa.
Kwa upande wake, Katibu Tawala wa mkoa wa Mwanza, Godwing Mtweve, amesema kuwa TFDA inawajibu wa kuhakikisha inalinda usalama na ubora wa bidhaa nchini ili kuhakikisha walaji wa mwisho (Wananchi) wanapata bidhaa ambazo ni salama kwa afya zao.
Leave a comment