HALMASHAURI ya mji Tunduma Imetenga kiasi cha Tshs Miloni 60 kujenga machinjio ya mifugo katika mtaa wa Msampa kata ya Chapwa wilayani Momba mkoani Songwe itakayowezesha mifugo kuchinjwa na kutunzwa eneo salama ukilinganisha na eneo lililokuwa likitumika kutokuwa salama. Anaripoti Ibrahim Yassin, Songwe…(endelea).
Akizungumza mwishoni mwa wiki na MwanaHalisi Online Ofisa mifugo wa halmashauri ya mji huo, Lusajo Mwalukasa alisema walipanga kutumia Sh 45 milioni kwenye ujenzi na Sh 15 milioni kulipa fidia kwa ajili ya eneo lakini uongozi wa kata umetoa eneo bure hivyo fedha hizo zitatumika kwenye maboresho ya ujenzi na kuifanya fedha ya ujenzi kuwa Sh 60 milioni.
Alisema fedha hizo ni za mapato ya ndani ambapo machinjio itakayojengwa itakuwa ya kisasa ikiwa na huduma zote muhimu zitakazozingatia hali ya usalama ili kulinda afya za walajix
Pia halmashauri itakusanya mapato yoke kwa uhakika na kudhibiti machinjio bubu zinazofanya kazi ya kuchinja mifugo kwa kificho.
Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji Tunduma, Phillimon Magesa alisema mbali na ujenzi huo pia kupitia mapato ya ndani kwa kipindi cha mwaka wa fedha wa 2022 hadi 2023 wamejenga Shule ya msingi Kokoto kwa Sh 800 milioni kati ya fedha hizo serikali kuu iliwapa Sh 400 milioni.
Alisema Zahanati ya Chipaka Imejengwa kwa Sh 500 milioni wao wameingiza Sh 290 milioni za mapato ya ndani na shule ya sekondari uwanjani Imejengwa kwa fedha za serikali.
Sambamba na hilo Magesa alisema, kwa sasa wapo kwenye mikakati ya kununua gari la Sh 68 milioni litakalokuwa na kazi ya kutembelea miradi ya maendeleo pamoja na gari la zimamoto.
Leave a comment