TUNDU Lissu, aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki amesema, yupo ‘fiti’ na kwamba sasa hatumii magongo hivyo hanasababu ya kuendelea kukaa Ulaya. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Lissu ambaye alikuwa Mnadhimu Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni ameelezea afya yake tarehe 30 Julai 2019, akisema afya yake inaimarika.
Hata hivyo amesema, matibabu yake yatakamilika tarehe 20 Agosti 2019, atakapokutana na timu ya madaktari kwa ajili ya vipimo vya mwisho na ushauri.
Lissu amesema, jana ilikuwa siku yake ya mwisho ya kutumia dawa, ikiwa ni mwezi mmoja umepita tangu alipoacha kutumia magongo kutembea.
“Kwa maelekezo ya madaktari wangu, jana ilikuwa siku ya mwisho ya mimi kutumia madawa ambayo nimeyatumia tangu siku niliposhambuliwa.
“Na jana (juzi) hiyo hiyo nilitimiza mwezi mzima tangu niache kutumia magongo. Ijapokuwa bado achechemea kwa sababu ya goti kutokukunja sawa sawa, sasa ninatembea bila msaada wa magongo,” amesema Lissu.
Ameeleza kuwa, akishafanyiwa vipimo vya mwisho, anaanza maandalizi ya kurudi Tanzania.
“Baada ya hapo itakuwa ni maandalizi ya kurudi makwetu. Hakutakuwa na sababu tena ya kitabibu ya mimi kuendelea kukaa Ulaya,” amesema Lissu.
Wakati huo huo, Lissu amezungumzia kuhusu hatua ya Bunge kumvua ubunge, amesema timu ya mawakili wake iko njiani kwenda Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga hatua hiyo.
“Sasa ninaweza kuwafahamisha kwamba mimi na timu ya mawakili wangu, tuko tayari kuingia Mahakama Kuu ya Tanzania. Tutafanya hivyo muda wowote kuanzia leo. Maandalizi yote yanayohitajika yamekamilika,” amesema Lissu.
Lissu amesema, anakwenda kuiomba Mahakama itoe ufafanuzi ya kwamba Spika Job Ndugai ana mamlaka kisheria kufuta ubunge wa mbunge pasipo kumueleza mhusika sababu za kumfuta ubunge.
“Tunataka kuiomba Mahakama Kuu itoe jibu la swali alilouliza Spika Ndugai na walio nyuma yake: Je, Spika wa Bunge la Tanzania ana uwezo kikatiba na kisheria, wa kufuta ubunge wa mbunge yeyote yule, kwa sababu yoyote ile, bila kumuuliza mbunge husika jambo lolote kuhusu sababu za kumfuta ubunge huo,” amesema Lissu.
Lissu amesema, atatoa taarifa kwa umma pindi kesi hiyo itakaposajiliwa, ili watu watakao penda kuhudhuria mahakamani kwa niaba yake, wafanye hivyo.
“Nitawajulisheni mara moja kesi hii itakaposajiliwa rasmi. Kama itawapendeza, nitawaomba mtakaopata nafasi kuhudhuria mahakamani, kwa niaba yangu, wakati wote kesi hiyo itakapokuwa inaendelea.
“Nilitaka kuwashirikisheni haya kwa leo. Nawashukuruni sana na Mungu awabariki sana,” amesema Lissu.
Leave a comment