KWA mara nyingine tena Rais Magufuli ametoa kauli yenye ukakasi mkubwa kwa Uhuru wa Mahakama. Anaandika Tundu Lissu, Ubelgiji … (endelea).
Iko hivi: Majaji na Mahakimu na watumishi wengine wa Mahakama sio miungu wala malaika. Ni binadamu na wanakosea.
Lakini kwa vile ni watumishi wa vyombo vya utoaji haki, Katiba na Sheria za nchi yetu – kama ilivyo kwa nchi nyingine – zimeweka utaratibu maalum wa kushughulikia masuala ya nidhamu na maadili ya Majaji na Mahakimu hao.
Kwa Majaji, both wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa, Rais anatakiwa kuteua Tume ya Uchunguzi ya Majaji angalau watatu, ili kuchunguza tuhuma za utovu wa maadili dhidi ya Jaji husika.
Kwa vile, kwa Katiba yetu ya sasa, Majaji wote ni wateule wa Rais, ili kulinda uhuru wa Tume ya Uchunguzi na kuhakikisha Jaji anayetuhumiwa anatendewa haki, Katiba imeweka masharti mawili muhimu.
Moja, jopo la uchunguzi lazima liwe na angalau Jaji mmoja atakayetoka katika mojawapo ya nchi za Jumuiya ya Madola.
Pili, uamuzi wa jopo la uchunguzi juu ya tuhuma dhidi ya Jaji husika ni wa mwisho, i.e. Tume ya Uchunguzi isipomkuta mtuhumiwa na hatia basi hawezi kuondolewa madarakani. Endapo ikimkuta na hatia basi Rais anaweza kumwondoa Jaji huyo madarakani.
Rais amepewa pia madaraka ya kumsimamisha Jaji mwenye tuhuma wakati uchunguzi dhidi yake unaendelea.
Hoja, kwa hiyo, ni kwamba kama kweli Rais Magufuli ana taarifa za utovu wa maadili dhidi ya Majaji anaodai kuwa nazo, basi afuate utaratibu uliowekwa na Katiba.
Hahitaji kumpelekea Jaji Mkuu mzigo huo. Aunde Tume ya Uchunguzi iliyoelekezwa na Katiba, halafu asubiri matokeo yake. Anaweza, kama anataka, kuwasimamisha kazi Majaji husika wakati uchunguzi unaendelea.
Kutuambia hadharani kwamba ana majina ya Majaji wanaokosea, halafu hafuati utaratibu wa kikatiba wa kuwashughulikia ni usanii hatari.
Kwa Rais kusema hivyo hadharani ni kuwafanya Majaji na Mahakimu wajisikie wanafuatiliwa mienendo yao na Rais muda wote. Huko ni kuwaweka kwenye hofu au mashinikizo kunakoweza kuhatarisha uhuru wao.
Rais aache tabia hii. Yeye sio Rais wa kwanza wa nchi yetu kukabiliwa na masuala ya nidhamu na maadili ya Majaji. Hata hivyo, tofauti na yeye, watangulizi wake hawakuwa wanatoa kauli za ajabu ajabu kama hizi.
Leave a comment