VIWANGO vikubwa vya kodi vimelalamikiwa katika mkutano wa Wakurugenzi wa Asasi za Kiraia (AZAKI). Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Wakizungumza katika nyakati tofauti kwenye mkutano huo wa siku mbili, ulioanza jana tarehe 13 Oktoba 2019 jijini Dodoma, AZAKI hizo zimeeleza serikali kutoza kiwango kikubwa cha kodi kwa asasi hizo, licha ya kutojiendesha kwa faida ni mateso.
Onesmo Olengurumwa, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) amesema, AZAKI nyingi hupewa fedha na wafadhili wa nje ya nchi, na kwamba mazingira magumu ya kodi yanaweza kuwakimbiza.
“Ukiweka mazingira magumu kama hayo, maana yake hata wafadhili watashindwa kutupa hela na wakishindwa, sisi ni wajiri wakubwa katika taifa hili ukicha serikali na sekta binafsi. Na sisi tunaajiri sana asasi ziko zaidi ya 50 nchi nzima,” amesema kuongeza:
“Tunaajiri watu wengi na hata zaidi ya serikali, tunalipa kodi, tunatoa fedha za kigeni, tunatoa elimu ya kiraia, tunatoa huduma mbalimbali za kijaamii. Unapozungumza asasi za kiraia ni sekta kubwa.”
Olengurumwa ameeleza, kuwa mchango wa AZAKI hapa nchini ni mkubwa hasa katika uboreshaji wa huduma za kijamii, hivyo serikali inabidi iziangalia kwa jicho la tatu.
“Mchango wa asasi ni mkubwa, lakini hakuna mahali ambako tunakotambuliwa.
Kama sekta iko hivyo halafu hakuna mikakati ya kuitambua ni changamoto kubwa. Sisi hatuna faida, unamwambia mtu alipe kodi wakati anapewa pesa ya mishahara na wafadhili. Pesa ya ziada anatoa wapi?
Ukizingatia hizi hela tunaziomba, hazikutokana na biashara zetu, wanatupa fedha tunazoomba kulingana na huduma zetu,” amesema Olengurumwa.
Richard Sambaiga, Mmwenyekiti wa Bodi AZAKI ameiomba serikali kuzipa nafuu AZAKI hizo katika masuala ya kodi, ili zilipe kulingana na mapato yake.
“Tutakapokuwa tunajadili fursa na changamoto za AZAKI, tuangalie namna gani kama sekta tunaweza tukachangia katika kodi ili kuona kiasi tulichochangia na kuomba kupunguziwa mzigo,” amesema Sambaiga.
Dk. Andrew Komba mshiriki wa mkutano huo, amesema suala la kodi kwa AZAKI ni changamoto ambayo hadi sasa haijapatiwa ufumbuzi
“Dhima ya mwaka huu ni nzuri. Kodi ni suala ambalo halijadiliwi kinagaubaga na huleta mtafaruku kidogo. Kama AZAKI tunapaswa kutambua tunafanya nini? Tupo wapi? Na tumetekeleza nini? Haya yanaonyesha wazi kuwa taifa linapata kiasi gani cha kodi,” amesema Dk. Komba.
Shogolo Msangi, akimuwakilisha Dk. Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango, amesema serikali hutoa misamaha ya kodi kupitia sheria zake, na kwamba iko tayari kufanya majadiliano na AZAKI ili kupata suluhu ya changamoto hiyo.
“Serikali inatoa misamaha ya kodi kupitia sheria zake, jambo la msingi ni kukidhi vigezo na masharti hakuna msamaha unaotolewa kama blanketi, na kama masharti hayatekelezeki basi tunawaalika tuyajadili,” amesema Msangi.
Leave a comment