WIZARA ya Maliasili na Utalii nchini Tanzania, imewahimiza wananchi walio karibu na hifadhi za wanyamapori, kutumia mbinu mbadala ili kuwadhibiti wasiingie kwenye maeneo yao na kusababisha uharibifu wa mali. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatano tarehe 28 April 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja, katika kipindi cha maswali na majibu, bungeni jijini Dodoma.
Masanja ametaja mbinu hizo kuwa ni, kilimo cha pili, ufugaji nyuki pembezoni mwa maeneo yao.
“Serikali inawahamasisha wananchi kulima shamba la zao la pilipili kando kando ya mashamba yao kwani zao hili limeonekana kuwa tishio kwa wanyama wakali na waharibifu kama Tembo,” alisema Masanja.
Naibu waziri huyo wa Maliasili na Utalii, amewashauri wananchi wanaoishi katika maeneo hayo, kutopanda mazao yanayowavutia wanyama pori kuvamia maeneo yao.
“Vilevile nawashauri kutokupanda mazao yanayowavutia Tembo kama vile katani, miwa, ndizi na matikiti. Pia waweze kutumia mafuta machafu yaliyochanganywa na pilipili na majivu ili kuzuia wanyama hao kusogea katika mashamba yao,” amesema Masanja.
Masanja alitoa uashauri huo akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Cecilia Pareso, aliyehoji mkakati wa Serikali katika kumaliza tatizo la wanyamapori kuvamia makazi ya watu na kuharibu mali za wananchi.
“Wananchi wanaoishi jirani na mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro wilayani Karatu, kwa muda mrefu wamekuwa wakipata hadha kubwa ya wanyama kuingia na kuvamia mashamba yao na wakati mwingine kujeruhi wananchi. Je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza tatizo hilo?” alihoji Pareso.
Pia, Pareso aliishauri Serikali ifanyie marekebisho Sheria inayosimamia fidia kwa wananchi wanaoharibiwa mali zao na wanyamapori wanaovamia makazi yao, akisema kwamba, sheria ya sasa imeweka viwango vidogo vya fidia, ambavyo haviendani na thamani ya mali zinazoharibiwa.
“Wanyamapori wanapoingia kwenye maeneo ya wananchi na wakaharibu mazao, fidia wanayolipwa hailingani na uharibifu uliotokea. Lakini hata fidia hiyo wanayolipwa inachukua miaka na miaka mpaka fidia hiyo waipate, Je ni lini serikali italeta marekebisho ya sheria bungeni ili kufanya marekebisho kwa wananchi kuweza kupata haki yao kwa jinsi inavyostahil?” Alihoji Pareso.
Leave a comment