KATIBU wa Chadema mkoani Ruvuma, Tasilo Bathlomew Milinga, leo Jumamosi, ametangaza kujiunga rasmi na Chama cha ACT-Wazalendo, huku akitaja sababu zilizopelekea kuchukua uamuzi huo ni kuunga mkono falasafa ya chama hicho, tume huru kuelekea katiba mpya. Anaripoti Mwandishi Wetu, Ruvuma…(endelea).
Tukio hilo limetokea leo Jumamosi, tarehe 18 Juni 2022, katika kongamano la tume huru kuelekea katiba mpya lililofanyika Songea, mkoani Ruvuma.
Mwanasiasa huyo amepokelewa na viongozi wajuu wa ACT-Wazalendo, akiwemo Mwenyekiti wake, Babu Juma Duni Haji.
Milinga amesema, ameamua kuvua nyadhifa zote alizokuwa nazo ndani ya Chadema, huku akidai hayuko peke yake, bali kuna wana Chadema wengine zaidi ya 150 waliofuata nyayo zake.
“Siku ya leo najivua rasmi vyeo vyote ndani ya Chadema, cheo cha kwanza katibu wa mkoa wa Ruvuma, wenye majimbo tisa. Najivua ujumbe wa mkutano mkuu wa taifa na mjumbe wa Baraza Kuu Taifa. Siko peke yangu, lakini nawakilisha wale wenzangu tuko zaidi ya 150. Lakini leo tuko 50 wengine hawajafika kwa sababu ya usafiri,” amesema Milinga.
“Ni chama kinachopigania kile inachokiamini, ni chama kinachotangza uhuru wa kweli na uhuru wa kujieleza na kinasimamia hilo, Uzalendo wa kweli wa chama hiki umetugusa wengi na kitaendelea kugusa wengi,. Ajenda hii ya tume huru ni ajenda mahususi sana na ni ajenda ambayo tuipambanie tume huru kwanza mengine yatafuta.”
Baada ya kujiunga na chama hicho, Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu, amesema wamefungua mlango kwa wanachama wa vyama vingine wanaotaka kujiunga nacho.
“Tasilo ameshapata kadi, ameshasajiliwa. Tunafungua milango kwa vyama vyote CUF, Chadema na vyama vingine wanaotaka kujiunga na ACT-Wazalendo,” amesema Ado.
Leave a comment