SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC), linatarajia kuanza majaribio ya mifumo ya umeme wenye ukubwa wa Volti 25,000, kwenye njia ya Reli ya Kisasa (SGR), kipande cha kwanza cha Dar es Salaam kwenda Morogoro.Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 23 Aprili 2022 na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano TRC, Jamila Mbarouk.
Taarifa ya Jamila imesema, umeme huo unatarajiwa kuanza kusambazwa kuanzia tarehe 27 Aprili mwaka huu.
Aidha, TRC imetoa tahadhari kwa wananchi wanaoishi pembezoni mwa miundombinu ya reli hiyo kuacha kufanya shughuli za kibinadamu, ikiwemo kukaa, kulala, kucheza na kutembea juu yake.
“Shirika linatoa tahadhari katika kipindi cha majaribio kwa wananchi na jamii inayoishi pembezoni mwa reli kuacha kufanya shughuli za kibinadamu katika njia ya reli ya kisasa. Kutopita katika maeneo ambayo si rasmi, kupanda nguzo zilizopo pembezoni mwa reli na kuacha kushika nyaya za kusambazia umeme ambazo zimegusa ardhi,” imesema taarifa ya Jamila.
Katika hatua nyingine, TRC imewataka wananchi kuchukua hatua za kiusalama wanapokuwa karibu na miundombinu ya SGR, ikiwemo kupita katika vivuko rasmi au sehemu zenye vibendera ili kuepuka ajali.
“Shirika la reli kwa kushirikiana na mkandarasi Yapi Merkezi wameanza kampeni maalumu yenye lengo la kutoa elimu ya namna ya kuzingatia na kuchukua tahadhari za kiusalama kupitia vyombo vya habari, mikutano ya hadhara kwa jamii inayoishi pembezoni kwa lengo la kukumbusha juu ya usalama wao na miundombinu ya reli,” imesema taarifa ya Jamila.
Leave a comment