MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA), imepongeza Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE), kwa kuanzisha klabu ya kodi kwa wanafunzi wanaosoma kwenye chuo hicho ambayo itaelimisha umma kuhusu umuhimu wa kulipa kodi. Mwandishi Wetu
Pongezi hizo zimetolewa leo chuoni hapo na Ofisa Mkuu wa Kodi wa mamlaka hiyo, Peter Shewiyo, wakati wa kongamano la 57 kuelekea mahafali ya chuo hicho yatakayofanyika siku ya Jumamosi.
Alisema klabu za kodi ni muhimu kwaajili ya kuelimimisha watanzania kuhusu umuhimu wa kulipa kodi ambayo hutumika kwaajili ya maendeleo kama ujenzi wa miundombinu ya zahanati, barabara, shule na huduma zingine muhimu.
“Naipongeza CBE kwa kweli mmefanya jambo jema na kubwa sana kuamua kuanzisha klabu ya kodi kwasababu wafanyakazi wa TRA peke yao hawawezi kuwafikia watanzania wote lakini kwa klabu hii ya CBE yenye vijana 100 nina uhakika watanzania 1,000,000 watapata elimu ya kodi,” alisema
Aliahidi kuwa TRA itashirikiana na klabu hiyo kwenye masuala mbalimbali ya kuelimisha umma kuhusu mambo ya kodi na itakuwa inawachukua kushiriki kwenye maonyesho mbalimbali nchini.
Kwa upande wake, Mkuu wa chuo hicho, Profesa Emmanuel Mjema aliwataka wahitimu wanaotarajiwa kuhitimu siku ya Jumamosi wasione kwamba wamemaliza shule na badala yake waone ni mwanzo wa kupiga hatua nyingine mbele kielimu.
Aliwataka watumie elimu hiyo kuonyesha mabadiliko kwenye jamii kwa kuanzisha biashara na kujiajiri wenyewe na kuajiri wenzao na kuachana na kasumba ya kutembea na vyeti mitaani kutafuta ajira.
Kwa upande wake, Naibu Mkuu wa chuo, Taaluma, Utafiti na Ushauri, Profesa Tandi Lwoga, alisema lengo la kufanya kongamano hilo ni kuwakutanisha wanafunzi waliopo na waliomaliza chuoni hapo kujadili mada mbalimbali za kitaaluma.
Alisema kongamano hiloni muhimu kwani huwawezesha wanataaluma hao kujadili mada zinazoigusa jamii na kiuchumi ili kuchangia na kufikia lengo kuu la nchi la kuwa taifa la viwanda kufikia mwaka 2025.
Alisema kwenye mahafali ya kesho Jumamosi wahitimu 1,605 watahitimu masomo yao na aliwambia kwamba wahitimu ni wengi na soko la ajira ni dogo hivyo wanapaswa kuwa wabunifu kwa kuanzisha baishara na kampuni zao wenyewe.
“Wanaotaka kuendelea na masomo warudi hapa kwasababu tunatoa hadi Shahada za Uzamili katika usimamizi wa biashara, ununuzi na ugavi, Tehama, jumla ziko program 13 tunazotoa shahada za uzamivu,” alisema Profesa Lwoga.
Leave a comment