MAMLAKA ya mapato Tanzania (TRA) Wilaya ya Chunya mkoani Mbeya imesema katika kuboresha mfumo wa ukusanyaji mapato, imeanza kutoa elimu kwa wachimbaji wadogo wa madini namna ya kutumia simu za mkononi kufanya malipo ya kikodi ili kurahisisha wachimbaji hao ambao ndio wengi katika wilaya hiyo kupata huduma za mamlaka hiyo ‘kiganjani’. Anaripoti Paul Kayanda, Mbeya …(endelea)
Hayo yamesemwa na Kaimu Meneja wa Mamlaka hiyo Osmund Mbilinyi wakati akizungumza kwenye maonesho ya kwanza ya teknolojia ya madini yanayoendelea kwenye viwanja vya Sinjiriri katika mkoa wa ki-madini Chunya.
Aidha, Meneja huyo amesema lengo kubwa la kuwapo kwenye eneo la maonesho ni kuhakikisha kuwa wanaendelea kutoa elimu kwa wachimbaji pamoja na wateja wake wengine hatua ambayo itarahisisha kusambaa haraka zaidi kwa elimu hiyo juu yam lipa kodi.
“Wachimbaji wadogo ni wadau wetu muhimu pamoja na wanunuzi wa madini hayo na kwamba sekta hiyo ndiyo inayotuingizia pato kubwa serikalini pamoja na mambo mengine sasa tunajikita kutoa elimu ya huduma za mlipa kodi kiganjani na watakuwa wanatumia huduma hiyo wao wenyewe pasipo kufuatwa na maafisa wa TRA,” amesema Mbilinyi.
Mbilinyi pia amesema TRA wapo katika kuboresha mfumo mpya wa mlipa kodi kiganjani ambao utamrahisishia mteja kufanya mwenyewe kila kitu.
Amesema TRA itapitia kile alichokifanya mteja mwenyewe na kuongeza kuwa mbali na maonesho hayo pia TRA inao utaratibu wa kutoa elimu kila baada ya miezi mitatu kwa kuwafuata wafanyabiashara wa madini pamoja na wachimbaji wenyewe kwenye maeneo yao ya kazi.
Amesema mkoa wa ki-madini Chunya una masoko ya dhahabu zaidi 20 ya ununuzi wa madini hayo na kwamba TRA inahakikisha inafikisha huduma karibu na wateja wake.
Ameongeza kuwa elimu inayotolewa ni kuanzia ukadiriaji, usajili, ujazaji wa taarifa za mauzo pamoja na shughuli zote ambazo zinaihusu TRA kwa wateja wake hasa wa madini ambao ni muhimu.
Leave a comment