CHAMA cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), kimeishauri Serikali ya Tanzania iwatumie mawakili wazawa, ili kuwaongezea ujuzi na kupunguza gharama. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Ushauri huo umetolewa leo Jumatano, tarehe 2 Februari 2022 na Rais wa TLS, Profesa Edward Hoseah akihutubia katika kilele cha maadhimisho ya siku ya sheria, yaliyofanyika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma na mgeni rasmi akiwa, Rais Samia Suluhu Hassan.
“Serikali kupitia Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na wizara husika, ione umuhimu wa kutumia TLS kwanza kabla haijakodi ujuzi wa kisheria kutoka nchi nyingine, hasa za magharibi,” amesema Profesa Hoseah.
Rais huyo wa TLS amesema “ni rai yangu, kuendeleza vipaji na ujuzi ulipo TLS utasaidia sana kupunguza ghamara kubwa za tegemezi kwa mawakili kutoka nchi za nje. Ni rai yetu kuwa Serikali iwatumie mawakili wenye uzoefu na ujuzi katika maeneo maalumu ambayo itafaidika na wataalamu wa ndani.”
Wakati huo huo, Profesa Hoseah ameshauri mawakili wa sekta binafsi na wa Serikali, waunganishwe pamoja ili waisadie nchi katika kutekeleza dira ya kukuza uchumi iliyojiwekea.
“Serikali kupitia wizara ya katiba na sheria ione umuhimu wa kuunganisha kada za mawakili wa umma na wale wa sekta binafsi kwani hauwezi kuwa na kada mbili katika tasnia moja,” amesema Profesa Hoseah na kuongeza:
“Tunahitaji kuwa na chama kimoja cha weledi wa shreia ili tuunganishe nguvu na utaalamu wetu, kulisaidia Taifa kufikia dira iliyojiwekea ya uchumi wa viwanda na maendeleo ya wananchi.”
Leave a comment