CHAMA cha Wanasheria Tanganyika (TLS), kimeitaka mahakama “iishi Katiba ya nchi, ilinde mamlaka yake kwa wivu wote na isiruhusu mamlaka yake kupokwa.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumatatu tarehe 1 Februari 2021, na rais wa chama hicho, Dk. Rugemeleza Nshalla katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini na miaka 100 ya Mahakama Kuu yaliyofanyika kwenye viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma.
Katika hotuba yake, Dk. Nshalla amesema, kucheleweshwa kwa kesi au kuahirishwa kutokana na kuchelewa kwa upelelezi, kumekuwa changamoto ya muda mrefu.
“Kuna watuhumiwa na mahabusu wengi wanaendelea kusota magerezani kwa kisingizio cha upelelezi kutokamilika, hii si sawa hata kidogo,” amesema Dk. Nshalla.
“Muda wa mwanadamu kuishi una ukomo wake, kila siku inayopita hairudi, ukimshika na kumweka ndani na kuendelea kumweka ndani, huna uwezo wa kumfidia muda huo wa uhuru uliomnyang’anya.
“Wewe unayemuweka ndani si Mungu ndiye anatupa uhai, njia pekee ya kuhakikisha unaheshimu uhuru wa mtu ni kuhakikisha upelelezi unapokuwa umekamilika au kama haujakamilika, anapewa dhamana, hivyo makosa yote yadhaminike,” amesema.
Leave a comment