SERIKALI kupitia Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknologia ya Habari imeunda kamati ya watu tisa itakayoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Azam Media Group, Tido Mhando kwa ajili ya kutathmini vyombo vya habari kiuchumi na kiutendaji. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 24 Januari, 2023, Waziri wa wizara hiyo, Nape Nnauye amesema amechukua hatua hiyo katika kutekeleza agizo la Rais Dk. Samia Suluhu Hassan baada ya kutoridhishwa na uchumi wa vyombo vya habari na masilahi ya waandishi wa habari.
Rais Samia aliagiza wizara hiyo kutafuta namna ya kushughulikia jambo hilo na kulifutia utatuzi.
Nape amesema kutokana agizo hilo Wizara imeunda kamati ya watu tisa inayongozwa na Tido Mhando ambaye ni mwenyekiti, Gerson Msigwa (Katibu) huku wajumbe wakiwa Dk. Rosse Rubeni, Joyce Mhavile, Sebastian Maganga, Bakari Machumu, Kenneth Sembeya, Jackiline Owiso na Richard Mwaikenda.
Nape amesema kamati hiyo inatakiwa kukamilisha kazi hiyo ndani ya miezi mitatu sawa na siku 90.
Amesema kazi kubwa ya kamati hiyo ni pamoja na kamati kufanya tathimini ya hali ya uchumi kwa vyombo vya habari kielimu na kiutendaji, hali ya waandishi wa habari na vyombo vya habari kuhusu ajira, vipato, mikataba na wawakilishi waliopo mikoani.
Aidha, kamati hiyo itatakiwa kutoa taarifa kwa jinsi utekelezaji wa mikataba na ajira vinavyoheshimiwa sambamba na pia kutafuta changamoto inayosababisha changamoto ya kiuchumi na changamoto ya kutekeleza kupitia vyombo vya habari serikali na wadau.
Nape amesema kazi ya kutafuta maoni ni ya watu wote hivyo watanzania pamoja na wanahabari wanatakiwa kutoa ushirikiano ikiwa ni pamoja na kutoa maoni kwa njia ya mtandao na mchakato wa mabadiliko ya sheria ya huduma ya vyombo vya habari umefikia pazuri na tayari umeishapelekwa kwa mwanasheria mkuu wa Serikali.
Leave a comment