MAWAKILI wanawake 40 kutoka mikoa mbalimbali nchini, wamepewa mafunzo ya kuendesha kesi zenye maslahi ya umma ‘kesi zakimkakati’ na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoanza leo Ijumaa hadi kesho Jumamosi, tarehe 4 Septemba 2021, yanafanyika katika Hoteli ya Seashell, Kijitonyama mkoani Dar ea Salaam.
Akizungumza wakati anafungua mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Chama cha Majaji wanawake Tanzania, Jaji Joaquine De-mello, amewataka mawakili hao kutumia mafunzo hayo kujiimarisha katika kufungua kesi za kimkakati.
“Wito wangu mkitoka hapa ni kutengenza kundi kubwa la utetezi wa mawakili wanawake, mkifanya maazimio mkubaliane kwamba hili ndio kundi mahsusi lenye nguvu moja ili waondokane na dhana ya kuwa wanawake hawawezi,” amesema Jaji De-Mello.
Jaji De-Mello ameipongeza THRDC kwa kuandaa mafunzo hayo, akisema yatasaidia kuongeza ushiriki wa wanawake katika kesi hizo.
“Ni ukweli kesi za maslahi ya umma ni njia madhubuti ya kukomesha ukiukwaji haki za binadamu dhidi ya umma, pamoja na hayo ushiriki wa wanawake ni mdogo ambapo hadi Machi mwaka huu, mawakili wanawake 3055 walisajiliwa lakini wanaoshirki bado wachache sana. Lakini mafunzo haya yatasaidia kuongeza ushiriki wao,” amesema Jaji De-Mello.
Naye Makamu wa Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika, Gloria Kalabamu, amewataka mawakili hao wasikatishwe tamaa na changamoto wanazokabiliana nazo wakati wa utekelezaji majukumu yao.
“Vikwazo vinavyotokea visitukwamishe bali tuyafanyie kazi, mfano unaweza katazwa usifungue kesi ya ndoa za utototoni sababu sio mwathirika lakini unaweza ukatafuta waathirika ukafungua kesi. Hivyo tusirudi nyuma tuwatafute wahusika ili tuwaeleze changamoto tunazopitia,” amesema Kalabamu.
Meneja Program wa THRDC, Remmy Lema, amesema wameandaa mafunzo hayo baada ya kuona mwitikio mdogo wa mawakili wanawake kushiriki katika kesi hizo za kimkakati.
“Lengo kubwa ni kuwajengea uwezo mawakili wanawake ili waweze kushiriki katika kesi zenye maslahi ya umma kitaifa na ngazi ya kikanda. Tuna mawakili wanawake 3055 lakini wanaoshiriki ni 92 tu ambayo ni chini ya asilimia 10. Hivyo kuna pengo kubwa la ushiriki wao,” amesema Lema.
Leave a comment