MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umeviomba vyombo vya ulinzi na usalama nchini viunde tume huru ya uchunguzi, ili kubaini chanzo cha mauaji ya watu wanne wakiwemo askari watatu, lililofanywa na kijana aliyefahamika kwa jina la Hamza Mohammed. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Tukio hilo lilitokea jana Jumatano, tarehe 25 Agosti 2021, katika makutano ya Barabara ya Ali Hassan Mwinyi na Kinondoni, karibu na Ubalozi wa Ufaransa nchini Tanzania, mkoani Dar es Salaam, baada ya kijana huyo kuanza kufyatua risasi hovyo na kuwauwa watu hao pamoja na kuwajeruhiwa watu sita.
Akizungumzia tukio hilo, leo Alhamisi, tarehe 26 Agosti 2021, Mratibu wa THRDC, amesema ni vyema tukio hilo lichunguzwe ili ijulikane kwa nini mtu huyo alifanya tukio hilo katika eneo lenye ulinzi mkali.
“Wito wetu iundwe tume huru ya uchunguzi, ili ufanyike uchunguzi kujua kwa nini mtu yule alifanya tukio lile hadharani, karibu na Kituo cha Polisi cha Salenda na ubalozi, ambalo ni eneo la usalama. Tukipata taarifa ilitokeaje tuna amini itakuwa sehemu ya kuzuia matukio ya namna hiyo,” amesema Olengurumwa.
Olengurumwa ameshauri tume hiyo iwe na majaji wastaafu na wadau kutoka asasi za kiraia.
“Tume iwe ya majaji wastaafu na makundi ya asasi za kiraia ili kubaini tatizo liko wapi, sababu mtu aliyehusika anafahamika, ndugu wako hapa hapa kama kuna jambo lilikuwa linaendelea Watanzania hatujui, tuelezwe chanzo kama hakutakuwa na sababu nyingine. Yule ni mhalifu mmoja lakini kama kuna mambo yalianza kupangika au wengine walianza kupanga itajulikana kwa nini alitokea barabarani,” amesema Olengurumwa.
Aidha, Olengurumwa amevishauri vyombo hivyo viwe na vifaa vya kisasa sambamba na mifumo madhubuti ya kiusalama, ili kubaini viashiria vya matendo hayo.
“Hili tukio linatupa ujumbe kwamba Jeshi la Polisi linatakiwa liwe na vifaa vya kisasa vya usalama na mifumo madhubuti ya kiusalama kama CCTV Kamera kwenye maeneo ya majiji. Hii ingesaidia Polisi kujua tukio linafanyika mahali fulani,” amesema Olengurumwa.
Jeshi la Polisi nchini Tanzania, limesema limeanzisha uchunguzi kuhusu tukio hilo, ambapo jana jioni lilizingira makazi ya aliyehusika na tukio hilo, yaliyoko Upanga jijini Dar es Salaam, kisha liliwachukua wanafamilia wake kwa ajili ya mahojiano.
Leave a comment