MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Bunadamu Tanzania (THRDC), umepewa msaada wa fedha kiasi cha Sh. 90 milioni na Shirika la International Center for Non-profit Law (ICNL), kutoka nchini Marekani, kwa ajili ya kutekeleza shughuli za utetezi wa haki za binadamu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar ea Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa kwa umma leo Ijumaa, tarehe 25 Februari 2022 na kitengo cha habari cha THRDC.
Taarifa ya THRDC imeeleza kuwa, fedha hizo zimetolewa baada ya INCL kuongeza mkataba wa ushirikiano na mtandao huo, ambao utaanza kutekelezwa mwishoni mwa Februari hadi Oktoba 202w.
“THRDC umeongeza mkataba wa kuendelea kushirikiana na shirika la INCL, mkataba huu una thamani ya Dola za Marekani 40,000, sawa na shilingi za kitanzania 90 milioni. Mkataba huu ni kwa ajili ya kuimarisha shughuli za utetezi wa haki za binadamu nchini Tanzania,” imesema taarifa ya THRDC.
Taarifa hiyo imesema kuwa, fedha hizo zitatumika katika mchakato wa utekelezaji mapendekezo yaliyokubaliwa na Serikali ya Tanzania, kwenye tathimini ya Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa (UN), kuhusu hali ya haki za binadamu nchini.
“Pia, zitatumika katika utoaji wa mafunzo mbalimbali kwa watetezi wa haki za binadamu nchini, ikiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali na waandishi wa habari. THRDC imekuwa ikifanya kazi na shirika la ICNL kwa muda mrefu, kama Wadau wakubwa wa haki za binadamu na wafadhili wa miradi mbalimbali ya mtandao,” imesema taarifa ya THRDC.
Leave a comment