MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), wameishauri Serikali iimarishe usalama wa viongozi wa Serikali za Mitaa, ili kudhibiti matukio ya kiusalama dhidi yao. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatano, tarehe 13 Oktoba 2021 na Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, siku moja baada ya tukio la mauaji ya aliyekuwa Afisa Mtendaji wa Mtaa wa Mbezi Msumi, mkoani Dar es Salaam, Kelvin Mowo, kutokea.
“Tunaomba na kushauri vyombo vinavyohusika visimamie masuala haya, tunashauri ofisi zetu za kata angalau kuwepo mgambo, mara zote wawepo kwenye mitaa yetu kuangalia hali ya usalama, ili kuboresha usalama wa watendaji wetu,” amesema Olengurumwa.
Mratibu huyo wa THRDC, ameitaka jamii kukemea vitendo hivyo ili visiendelee kushamiri.
“Tunapaswa kukemea kitendo hiki sababu ni cha kidhalimu, kinakwenda kinyume na misingi ya utawala bora na haki za binadamu,” amesema na kuongeza:
“Ili kuzingatia sheria na taratibu za haki za watu, tunapaswa kuona hili suala halipaswi kuwepo katikati yetu. Tunataka tuwe na jamii ambayo imestaarabika, jamii ambayo ikipata tatizo lolote inafuata hatua za kisheria.”
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Jeshi la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro, tukio hilo la mauaji limetokea asubuhi ya tarehe 11 Oktoba 2021, wakati marehemu Mowo akisikiliza mgogoro wa ardhi.
Wakati Mowo akisikiliza mgogoro huo akiwa ofisini kwake, watu wanne wasiojuliakana waliingia kisha mmoja alitoa panga na kumshambulia.
Na kumsababishia majeraha makubwa yaliyokatisha uhai wake, akiwa njiani kuelekea hospitalini.
Kamanda Muliro alisema watu watatu wanashikiliwa na Jeshi la Polisi, kuhusiana na tukio hilo na kwamba taratibu za upelelezi zikikamlika watafikishwa mahakamani.
Leave a comment