SIKU 100 za uongozi wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, zinaelezwa kutoa ahueni katika Mshirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) nchini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika mahojiano na MwanaHalisi Online kuhusu siku 100 za Rais Samia madarakani, zilizohitimishwa tarehe 27 Juni 2021, viongozi wa taasisi hizo wameelaza, siku hizo zimerejesha uhuru wa kufanya kazi.
Rais Samia aliapishwa kuwa Rais wa Tanzania tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, kilichotokea tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam.
Akizungumzia siku hizo, Mratibu Mkazi wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), Onesmo Olengurumwa, amesema zimeleta matumaini na muonekano mpya wa Kitaifa.
“Kama mwanaharakati na mtetezi wa haki za binadamu, naziona ni siku za kheri, nafuu na matumaini. Ni siku za furaha kwa Watanzania, siku za muonekano mpya wa kitaifa katika maeneo mbalimbali ya kijamii.
“Imekuwa kipindi cha tiba kwa Watanzania wengi, imerudisha mshikamano wa kitaifa, nafasi ya Watanzania katika utetezi wa haki za binadamu imerudi, tunaweza kusema bila kuwa na hofu,” amesema Olengurumwa.
Wanaharakati huyo ameeleza, kwa sasa NGO’s zinafanya kazi kwa ukaribu na taasisi za serikali, tofauti na ilivyokuwa nyuma.
“Siku 100 zimetugusa kwa kaisi kikubwa, sasa hivi taasisi mbalimbali za kiserikali zinafanya kazi bila uoga na asasi. Huko nyuma ilikuwa kufanya kazi na asasi kama kujichongea.
“Sasa hivi tunafanya kazi kwa uhuru, mawaziri tuko nao vizuri hatuna changamoto yoyote. Taasisi za serikali zina mfumo wa kushirikisha taasisi, imetupa fursa kufanya kazi na viongozi wetu.”
Mratibu huyo wa THRDC amesema, mazingira ya sasa yanatoa nafasi kubwa kwa watetezi wa haki za binadamu nchini, kufanya shughuli za maendeleo kwa wananchi.
“Tunaoshughulika na masuala ya haki za binadamu mfano THRDC, inazichukulia siku hizi kwa upana mkubwa kwa sababu mazingira tuliyokuwa nayo kabla siku 100 na mazingira tuliyonayo katika siku hizi 100,” amesema Olengurumwa na kuongeza:
“Tunaona kama Taifa tunakwenda kuwa na mazingira mazuri ya kufanya uteetezi wa haki za binadamu, kushirikiana na Serikali katika majukumu yetu ya kutetea na kusukuma gurudumu la maendeleo.”
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Tanzania (LHRC), Anna Henga, amesema siku 100 za Rais Samia zimeleta uhuru kwa makundi mbalimbali, hasa watetezi wa haki za binadamu na wanahabari.
“Siku 100 zimeleta matumaini kwa watetezi, tumeona watu wamekuwa huru kuwasiliana, uhuru wa kupata habari umerudi. Tumeona mtu akipata habari bila wasiwasi, ametoa mwanya kwa watu kutoa kero zao, wasibanwe na viongozi kutoa kero zao,” amesema Henga.
Rais Samia S,Hassan katika siku 100 ameonyesha mabadiriko nakubwa mno,amerejesha furaha kwa Watanzania
Mwenyezi Mungu ampe Maisha marefu.
Mungu ibariki Tanzania