TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania, imetoa sababu za kuchelewa kutoa vibali vya utoaji elimu ya mpiga kura na uangalizi wa uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2020, kwa Asasi za Kiraia (AZAKI). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tarehe 27 Novemba, 2019, NEC ilitoa taarifa ya kuyataka mashirika yasiyo ya kiserikali yenye nia ya kuomba vibali vya kutoa elimu ya mpiga kura na kuangalia uchaguzi kuwasilisha maombi yao katika ofisi za tume hiyo.
Lakini, juzi Jumapili tarehe 17 Mei, 2020, Onesmo Olengurumwa, Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), aliilalamikia NEC kwa kuchelewa kutoa majibu ya AZAKI, zilizoomba kushiriki shughuli hizo.
Olengurumwa alisema changamoto hiyo inaweza kukwamisha maandalizi ya AZAKI hizo, kwa kuwa kupata fedha za kutekeleza shughuli zao kutoka kwa wafadhili, ambao hawatoi fedha hadi asasi hizo zipate vibali.
“AZAKI hazina fedha, hutegemea fedha kutoka kwa wafadhili, ambao hutoa kwa AZAKI zenye vibali vya kuangalia uchaguzi kutoka kwenye mamlaka husika. Lakini tangu mwezi Januari mwaka huu asasi za kiraia zimeomba vibali kutoka NEC, lakini haijatoa majibu,” alisema Olengurumwa.

Akizungumza na MwanaHALISI ONLINE kwa simu leo tarehe 19 Mei, 2020, Dk. Wilson Charles, Mkurugenzi NEC, amesema vibali hivyo havijatolewa kutokana na mchakato wa kuzichambua AZAKI zilizokidhi vigezo, haujakamilika.
Hata hivyo, Dk. Charles amesema mchakato huo uko mbioni kukamilika na kuahidi kwamba AZAKI zitakazokidhi vigezo, zitapewa vibali ndani ya kipindi cha mwezi mmoja kutoka sasa.
“Hatujatoa mpaka sasa hivi vibali, sababu tume ina utaratibu, ina michakato inaendelea nayo. Tuko kwenye hatua za kufanya upembuzi wa maombi yao, hivi karibuni haitapita mwezi mmoja watapa taarifa,” amesema Dk. Wilson.
Kuhusu maandalizi ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020, Dk. Wilson amesema yanaendelea vizuri na kwamba kwa sasa NEC imeanza kuandaa vifaa vya uchaguzi nchi nzima.
“Tunaendelea na utaratibu sababu uchaguzi ni mchakato, tuko kwenye taratibu za kukamilisha uboreshaji daftari la wapiga kura, ambapo kwa mujibu wa kisheria tumeboresha mara mbili,” amesema Dk. Charles.
Dk. Charles amesema NEC inasubiri bunge livunjwe, ili lianze zoezi la uteuzi wa wagombea katika nafasi mbalimbali kwenye uchaguzi huo, ambalo litafanyika ndani ya siku 25.
“Siku bunge likishavunjwa kisheria tunaanza mchakato wa kuanza masuala ya uteuzi na baada ya uteuzi kampeni na baada ya kampeni ni uchaguzi. Likishavunjwa kisheria na baada ya uteuzi, ndani ya siku 60 mpaka 90 uchaguzi tayari,” amesema Dk. Charles na kuongeza:
“Tunaendelea na maandalizi, wananchi wajiandae na uchaguzi. Maandalizi ya kuandaa vifaa vya uchaguzi yanaendelea nchi nzima.”
Kwa mujibu wa taarifa ya Spika wa Bunge, Job Ndugai aliyoitoa jana Jumatatu tarehe 18 Mei, 2020 mjini Dodoma, shughuli za mhimili huo zinatarajia kufikia tamati tarehe 19 Juni, 2020, ambapo Rais John Magufuli, anatarajiwa kulivunja.
Leave a comment