MTANDAO wa Jinsia Tanzania (TGNP) umekutana na wadau pamoja na Wabunge wanawake vinara wa jinsia bungeni Dodoma na kuwapa mafunzo ya umuhimu wa bajeti kuanzia ngazi ya halmashauri hadi bajeti kuu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma… (endelea).
Mafunzo hayo yenye mrengo wa kijinsia ni mahususi katika kuwanufaisha wanawake na makundi yaliyoko pembezoni ili kuondoa changamoto zinazowasibu kwenye upande wa afya, elimu, maji, haki ya uchumi, kilimo na ukatili wa kijinsia.
Mwezeshaji wa mafunzo hayo kutoka TGNP, Deogratius Temba amesema mafunzo hayo ni muhimu kwa kuwa yanaibua majadiliano chanya pamoja na kuzipatia ufumbuzi changamoto za masuala mbalimbali ya kijinsia hasa kwa kundi la wanawake, watoto na kundi la wenye ulemavu.
Temba amesema TGNP imeendelea kushirikiana na makundi mbalimbali katika kujadili bajeti kila mwaka kwa mrengo wa kijinsia na kwamba lengo ni kuwa na maendeleo endelevu yenye kujumuisha ustawi wa makundi yote na kudumisha haki za msingi za binadamu.
Amesema TNGP inafanya jitihada kuboresha sekta za huduma kwa jamii ambazo kwa kiwango kikubwa zinawagusa wanawake moja kwa moja.
“Hii ni pamoja na kuboresha miundombinu ya huduma za afya na elimu ili kuamsha ari kwa Serikali kutenga bajeti yenye kulenga na kuhamasisha utoaji wa bima za afya kwa gharama nafuu kwa wajane wenye uhitaji, wazee na wanawake na kaya masikini nchini,” amesema.
Aidha, Mwenyekiti wa Chama cha wabunge wanawake, Margaret Sitta amesema kwa kushirikiana na wabunge wenzake vinara wa jinsia watahakikisha mara kwa mara wanaisemea bajeti hiyo ya mrengo wa kijinsia.
Amesema hali hiyo itaongeza uwekezaji katika kutoa elimu ya umuhimu na namna ya kuzuia magonjwa kwa watu wa pembezoni ili kupunguza gaharama za matibabu ya magonjwa yanayozuilika.
Pia itaimarisha ujenzi wa uchumi shindani wa viwanda na kusisitiza kuwa maendeleo ya watu yanahitaji nguvu kazi ya afya bora.
“Tunawapongeza wenzetu wa TGNP kwa kutushirikisha sisi pamoja na akina mama hawa na walipokuja hapa.
“Niliwauliza kwamba je, wawakilishi wenu wabunge wanayajua haya, wamesema wanayajua kwa hiyo mimi nilikuwa nafikiri ni vizuri kushirikiana na wabunge wa maeneo yao kwa sababu taarifa ya majimbo tunapeana pengine taarifa wananchi hawana lakini wabunge wa majimbo wanajua nini kinafanyika katika maeneo yao,” amesema.
Naye mmoja wa wawakilishi wa mafunzo hayo na mdau wa masuala ya kijinsia kutoka Wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga, Neema Maige amesema anatamani kuona majadiliano yaliyofanyika kwenye mafunzo hayo yanazaa matunda kwa kuwa amechoshwa na changamoto ya uhaba wa maji katika wilaya yao.
Amesema ikiwa idara za maji za mikoa zitawezeshwa, hali ya upatikanaji wa maji kwa wajane, wazee, kwa tozo za viwango vya chini kabisa, au hata bila tozo yoyote itawezekana.
Leave a comment