WAKALA wa Uhifadhi wa Misitu Tanzania (TFS), imefanikiwa kutoa ajira kwa watu 400 kwenye shamba la miti la Iyondo Mswima wilaya Ileje mkoani Songwe. Anaripoti Ibrahim Yassin, Ileje … (endelea).
Pia Wakala huo umetoa elimu ya uhifadhi wa mazingira kwa wananchi 600 wanaouzunguka msitu huo.
Hayo yamebainishwa leo tarehe 17 Februari 2023 na kaimu Mhifadhi wa shamba hilo Jovan Emmanuel kwenye ofisi za TFS zilizopo Katengele wakati wa ugawaji wa miche ya miti kwa wananchi wanaozunguka shamba hilo zoezi lililofanywa na Mkuu wa Wilaya hiyo Farida Mgomi.
Jovan amesema ofisi ya TFS imekuwa na utaratibu wa kugawa miche ya miti kwa wananchi wa vijiji vinavyolizunguka shamba hilo lenye ukubwa wa hekta 5418 ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wananchi hao juu ya umuhimu wa uhifadhi mazingira.
“Kwa mwaka wa fedha 2022/2023 ofisi ya shamba la miti Iyondo Mswima linatarajia kugawa miche ya miti 30,000 ikiwa ni kutimiza lengo la kushirikiana na jamii inayowazunguka kutunza mazingira”, amesema Jovan.
Kwa upande wake mkuu wa wilaya hiyo Farida Mgomi akizungumza wakati wa kugawa miche kwa wananchi hao amesema wanataka wananchi kujiepusha na uharibifu wa mazingira ikiwepo kufanya shughuli za kibinadamu kama kulima, kuchunga mifugo, kuchoma mkaa na kuchoma misitu hovyo kwani shughuli hizo zinaharibu uoto wa asili uliopo.
Mgomi amesema kila mwananchi wa Ileje anao wajibu wa kulinda mazingira kwa kushirikiana na TFS lengo likiwa ni kuendeleza takwa la kisheria la kila kaya kupanda miti ikiwepo ya kivuli, matunda, na mbao kwa ajili ya kujiingizia kipato.
“Kila mwananchi na taasisi zitakazonufaika kupata miche hiyo izingatie upandaji kitaalamu ili isiharibike kwani tusipozingatia hayo tutaharibu miche hiyo na kupoteza lengo la TFS,” amesema Mgomi.
Leave a comment