WAOKOAJI nchini Uturuki na Syria wameendelea na kazi ya kupekua vifusi kuwatafuta manusura au kuopoa miili ya watu waliopoteza maisha kutokana na tetemeko la ardhi lililoyakumba mataifa hayo mawili Jumatatu wiki hii.
Juhudi hizo zinafanyika wakati idadi ya vifo vilivyosababishwa na janga hilo la asili ikiongezeka na kufikia watu 24,000 huku mamia kwa maelfu wengine wakipoteza maeneo ya kuishi. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa Wetu … (endelea).
Sehemu kubwa ya vifo na athari mbaya ya tetemeko hilo la ardhi la siku ya Jumatatu imeshuhudiwa kwenye mji wa mashariki mwa Uturuki wa Kahramanmaras.
Mji huo ndiyo ulitikishwa vibaya na dhahama hiyo ya asili iliyoporomosha majengo, kuharibu miundombinu na kuvuruga maisha ya watu ambao hadi Jumapili iliyopita walikuwa wakiishi maisha ya kawaida kwenye eneo hilo.
Mji huo unapatikana kwenye mkoa wa pembezoni mwa Uturuki ambao umekuwa makazi ya watu waliokimbia machafuko ndani ya Uturuki na nchi jirani ya Syria.
Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuwa karibu watu 870,000 hivi sasa wanahitaji msaada wa haraka wa chakula nchini Uturuki na Syria. Nchini Syria pekee, watu wasiopungua milioni 5.3 huenda wamepoteza maeneo yao ya makaazi.
MIUJIZA YAJITOKEZA
Kwenye maeneo ya maafa, miujiza imeendelea kushuhudiwa hata baada ya saa 100 tangu kutokea kwa tetemeko la ardhi lenye ukubwa wa 7.8 katika kipimo cha Richter.
Mwanamke mmoja mjamzito kwa jina la Zahide Kaya amepatikana akiwa hai kutoka kwenye kifusi cha jengo baada ya saa 115 tangu kutokea kwa tetemeko.
Kwa mujibu shirika la habari la Uturuki, mwanamke huyo ameokolewa kwenye wilaya ya Nurdagi iliyopo katika jimbo la Gaziantep, kusini mashariki mwa Uturuki.
Mtoto wake wa kike mwenye umri wa miaka sita naye aliokolewa kutoka kwenye vifusi saa moja baadaye. Mama huyo amekutwa na majeraha kadhaa mwili na alipelekwa mara moja hospitali.
Hata hivyo, hali ya hewa ya baridi kali imesababisha ugumu wa maisha kwa wale walionusurika na hata vikosi vya waokoaji.
Leave a comment