NI takribani siku ya tano tangu kutokea kwa tetemeko la ardhi nchini Haiti. Anaripoti Victoria Mwakisimba, TUDARCo kwa msaada wa mashirika ya kimataifa (endelea).
Tetemeko hilo lenye ukubwa wa kipimo cha Richter 7.2 lilipiga upande wa mji mkuu wa Port na kuharibu vibaya majengo makubwa yakiwemo makanisa, shule na makazi ya watu na miundombinu.
Nchi hiyo imekumbwa na janga hilo ikiwa bado ipo kwenye wingu zito la mauaji ya raisi wao Jovenel Moise yaliyo tokea Julai, 2021, aliyeshambuliwa akiwa katika makazi yake.
Wananchi wamekuwa wakilala nje baada ya makazi yao kubomolewa na wengine wakiwa na hofu ya tetemeko hilo kuharibu makazi yao tena.
Mataifa mbalimbali ikiwemo Marekani na Argentina yameahidi kutoa msaada kwa nchi ya Haiti. Rais wa Marekani, Joe Biden amekwisha kuagiza Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) kufanya tathimini ya janga hilo.
Shirika la Usalama wa raia limetoa taarifa majengo 13,600 yameporomoka na zaidi ya majengo 13,700 yameharibiwa huku mamia ya watu wamefunikwa na vifusi na shughuli za uokoaji zinaendelea na zaidi ya watu 5,700 wamejeruhiwa.
Aidha Marekani imetuma kikosi cha waokoaji 65 wenye zana na vifaa vya kimatibabu kujiunga na jeshi la uokoaji nchini Haiti.
Tukio hilo liliwahi kutokea pia mwaka 2010 ambapo tetemeko lenye ukubwa wa 7.0 katika kipimo cha Richter lilipiga nchi hiyo ya kisiwa na kusababisha vifo 200,000 na makazi ya raia milioni 1.5 yaliharibiwa.
Pia, mfumo wa sekta ya afya uliharibiwa kwa asilimia 60 na kuifanya serikali ya kisiwa hicho kuwa kwenye wakati mgumu.
Aidha, kama vile Chile, Peru,Venezuela pamoja na Umoja wa Mataifa (UN) yametoa ahadi kuisaidia Haiti.
Waziri Mkuu wa Haiti Ariel Henry ametangaza hali ya hatari kwa mwezi mzima na kuomba raia waonyeshe mshikamano.
Leave a comment