MKURUGENZI wa lebo ya Wasafi Classic Baby (WBC), Naseeb Abdul ‘Diamond Platnums’ amesema mkali mwenzie wa Bongo fleva kutoka katika lebo hiyo, Raymond Mwakyusa ‘Rayvanny’ ameingiza kiasi cha Sh milioni 230 katika mauzo ya wimbo wake wa ‘Tetema’.
Katika wimbo huo wa ‘Tetema’, Rayvanny amefanya Remix na msanii kutoka Colombia anayekwenda kwa jina la Maluma. Anaripoti Calvin Nyorobi …(endelea).
Pia Diamond au Mondi amesema katika lebo hiyo ya Wasafi, Rayvanny ndiye msanii wa pili anayeingiza mapato makubwa huku nafasi ya kwanza akiishika mwenyewe.
Mondi ametoa kauli hiyo leo tarehe 14 Machi, 2022 katika mahojiano aliyofanya kwenye kipindi cha The Switch kinachorushwa na Wasafi FM.
Aidha, akizungumzia suala la mirabaha iliyoanza kutolewa hivi karibu na Serikali ya Tanzania, Mondi ametoa wito kwa viongozi kuangalia mchanganuo wa mirahaba hivyo kwa umakini ili wasiitie aibu serikali.
Amesema aliwahi kwenda Chama cha Hakimiliki Tanzania (COSOTA) kufuata mrabaha wake akapewa Sh 30, 000 lakini cha ajabu msanii mwenzie alipewa kitita cha noti za kutosha.
Kuhusu Tuzo za Tanzania, Mondi amesema hapambani kupata tuzo za ndani kwani anaamini waandaji hawawezi kumpatia tuzo hizo hata kama anastahili kupewa.
Ameenda mbali zaidi na kudai kuwa usimamizi wa tuzo hizo za Tanzania ni mbovu.
Leave a comment