MWENYEKITI wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, amesema mchakato wa marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari ya 2016, unakwenda vizuri Kwa kuwa Serikali imechukua sehemu kubwa ya mapendekezo ya wadau kwa ajili ya kuandaa muswada wa marekebisho yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Balile ametoa taarifa hiyo Leo Jumapili, tarehe 27 Novemba 2022, akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maendeleo ya mchakato huo, baada ya hivi karibuni Serikali kukutana na wadau kwa ajili ya kufanya mapitio ya mwisho ya mapendekezo kuhusu marekebisho ya Sheria hiyo.
“Kwa hakika sisi kama wadau wa habari tumefika hatua nzuri na hata kuwa na matumaini chanya hasa baada ya kikao Cha mwisho kati ya wanahabari na Serikali.Wakati unaofuata ni wa Serikali na hatua zake katika kuelekea mabadiliko ya Sheria ya habari. Lakini mpaka hapa tulipofika tunaamini Kuna jambo linakwenda kutokea,” amesema Balile.
Balile amesema kuwa, kitendo cha Serikali kushirikisha wadau ikiwemo taasisi za habari nchini, katika mchakato wa marekebisho hayo, kimerahisisha kwenda vizuri.
“Kwa kuwa wadau wa habari tunapigania kitu kimoja, tuliamua Kwa pamoja kujiweka chini ya mwamvuli tunaouaita CoRI (Wadau wa Kupata Habari). Jambo hili limerahisisha Serikali kujua wanazungumza na watu gani, tusingekuwa pamoja pengine mambo yasingekwenda Kwa namna tulivyoona,” amesema Balile.
Hivi karibuni, Nape Nnauye, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari amewahakikishia wadau wa habari kwamba, serikali itakamilisha mchakato wa mabadiliko ya vipengele vya sheria ya habari.
Alitoa kauli hiyo kwenye kikao chake na wadau wa Haki ya Kupata Habari (CoRI), tarehe 21 Novemba 2022, jijini Dar es Salaam.
Nape alisema, serikali imepokea maoni yao kuhusu mapendekezo ya marekebisho ya Sheria ya Huduma za Habari Na 12 ya 2016.
“Niwahakikishie kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, inayo nia ya dhati katika jambo hili. Nimekuja mwenyewe kuwasilikiliza na imani yangu ni kuona sekta inaendelea kukua” amesema.
Miongoni mwa mapendekezo ya CoRI kwa serikali ni pamoja na mamlaka haya ya Mkurugenzi wa Habari (MAELEZO) yafutwe na kiundwe chombo ambacho pamoja na mambo mengine, kitashughulikia masuala ya usuluhishi yanapotolewa malalamiko dhidi ya chombo cha habari, badala ya kazi hiyo kufanywa na mtu mmoja.
Wadau wanataka marekebisho dhidi ya kifungu cha 6 (e) kinachoelekeza magazeti kupatiwa leseni badala ya usajili wa moja kwa moja.
Pia wadau hao wanapendekeza magazeti yasiendeshwe kwa kupewa leseni, badala yake yapewe usajili wa kudumu au wa muda mrefu, ili kudhibiti changamoto ya ufutwaji holela wa leseni na kuvutia wawekezaji.
Leave a comment