JUKWAA la Wahariri Tanzania (TEF), limeshauri Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi wa haraka, ili kubaini chanzo na watu waliohusika kumuua Blandina Sembu, aliyekuwa mtangazaji wa Kituo cha Televisheni cha ITV. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana, Deodatus Balile ambaye ni kaimu mwenyekiti wa jukwaa hilo, ameeleza kushtushwa na taarifa za kifo cha hicho.
“Jeshi la Polisi nchini liongeze nguvu katika uchunguzi wa tukio hilo la kinyama, ili kuhakikisha wahusika wake wanapatikana na kufikishwa katika vyombo vya
sheria. Tunahimiza uchunguzi wa haraka kwasababu chanzo na sababu za mauaji ya Blandina bado haijafahamika.
“Kutofahamika huko, kunawaweka waandishi wa habari nchini na hasa wa ITV katika wasiwasi kuhusu usalama wa maisha yao, hali ambayo kimsingi inaathiri utendaji wa kazi zao za kila siku,” imeeleza taarifa hiyo.
Tarehe 28 Machi 2021, mwili wa Blandina ulitupwa mbele ya Baa ya Maryland saa tano usiku, ambapo taarifa zaidi zinaeleza, mauaji yake yalifanyika sehemu nyingine.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa Kinondoni, Ramadhan Kingai, gari moja aina ya Noah Toyota iliegesha eneo la baa hiyo na kuwasha taa za kuegesha gari kwa dharura (hazards), kisha kuondoka ndani ya dakika mbili.
Kingai alisema, Blandina alitupwa katika eneo hilo akiwa tayari amefariki dunia.
Hata hivyo, TEF imetoa wito kwa waandishi wa habari nchini, kuchukua hadhari wanapokuwa katika utekelezaji wa majukumu yao na shughuli nyingine nje ya Kazi, ili kuhakikisha wanakuwa salama dhidi ya madhara yoyote yanayoweza kuhatarisha uhai na maisha yao.
“Usalama wa Mwandishi wa Habari, unapaswa kuanza na mwandishi wa Habari mwenyewe,” imeeleza taarifa hiyo.
Leave a comment